hotuba ya mwenyekiti wa tume ya mabadiliko ya katiba mhe joseph s. warioba, ripoti ya tume kwa rais...

Upload: muhidin-issa-michuzi

Post on 04-Jun-2018

301 views

Category:

Documents


2 download

TRANSCRIPT

  • 8/13/2019 Hotuba Ya Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba Mhe Joseph S. Warioba, Ripoti ya Tume kwa Rais Kikwet

    1/23

    1

    HOTUBA YA MWENYEKITI WA TUME YA MABADILIKO YA

    KATIBA, MHE. JOSEPH S. WARIOBA WAKATI WA KUKABIDHI

    RIPOTI YA TUME KWA RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA

    TANZANIA, MHE. DKT. JAKAYA MRISHO KIKWETE NARAIS WA ZANZIBAR MHE. DKT. ALI MOHAMED SHEIN;

    TAREHE 30 DESEMBA, 2013, DAR ES SALAAM

    ________________

    Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya

    Muungano wa Tanzania;

    Mheshimiwa Dkt. Mohamed Gharib Bilal, Makamu wa Rais wa

    Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;

    Mheshimiwa Dkt. Ali Mohamed Shein, Rais wa Zanzibar naMwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi;

    Mheshimiwa Mizengo Kayanza Peter Pinda, Waziri Mkuu;

    Mheshimiwa Maalim Seif Sharif Hamad, Makamu wa Kwanza waRais wa Zanzibar;

    Mheshimiwa Balozi Seif Ali Iddi, Makamu wa Pili wa Rais waZanzibar;

    Mheshimiwa Anne Makinda, Spika wa Bunge la Jamhuri yaMuungano wa Tanzania;

    Mheshimiwa Pandu Ameir Kificho, Spika wa Baraza laWawakilishi;

    Mheshimiwa Mohamed Chande Othman, Jaji Mkuu wa Tanzania;

    Mheshimiwa Omar Othman Makungu, Jaji Mkuu wa Zanzibar;

    Mheshimiwa Mzee Ali Hassan Mwinyi, Rais wa Pili wa Jamhuri ya

    Muungano wa Tanzania;

  • 8/13/2019 Hotuba Ya Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba Mhe Joseph S. Warioba, Ripoti ya Tume kwa Rais Kikwet

    2/23

    2

    Mheshimiwa Mzee Benjamin Mkapa, Rais wa Tatu wa Jamhuri ya

    Muungano wa Tanzania;

    Waheshimiwa Viongozi wote mliopo hapa;

    Waheshimiwa Mabalozi;

    Ndugu wananchi;

    Mheshimiwa Rais,

    Kwa makubaliano na Mheshimiwa Rais wa Zanzibar, tarehe 6 Aprili,

    2012 ulituteua kuwa wajumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba,

    ulituapisha tarehe 13 Aprili na tulianza kazi tarehe 2 mei, 2012. Tulikuwa

    34, yaani wajumbe 32 na Katibu na Naibu Katibu. Leo tuko hapa 32.

    Kama inavyofahamika tulimpoteza mjumbe mmoja, Dr. Sengondo Mvungi

    katika mazingira ya kusikitisha.Mungu aiweke roho yake mahali pema

    peponi. Mjumbe mwingine, ndugu John Nkolo, hayuko hapa kutokana na

    matatizo ya kiafya. Hali yake inaendelea vizuri. Vile vile mjumbe wa

    sekretariati ndugu Onorius Njole aliugua wakati Tume ilipokuwa

    inasimamia Mabaraza ya Katiba. Naye pia hali yake inaendelea vizuri.

    Mheshimiwa Rais,

    Sheria ya Mabadiliko ya Katiba ilitoa miezi kumi na nane kwa Tume

    kukamilisha kazi yake. Sheria pia ilitoa nafasi ya Tume kuongezewa

    muda usiozidi miezi miwili na Tume iliomba muda huo na ulitukubalia.

  • 8/13/2019 Hotuba Ya Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba Mhe Joseph S. Warioba, Ripoti ya Tume kwa Rais Kikwet

    3/23

    3

    Kazi tuliyopewa tumeikamilisha na leo tupo tayari kukabidhi kwako

    na kwa Mheshimiwa Rais wa Zanzibar Ripoti yetu kama sheria

    inavyoelekeza. Ripoti tunayoikabidhi inaambatana na taarifa saba

    zifuatazo:-

    (i) Maoni ya Wananchi kuhusu Mabadiliko ya Katiba ya Jamhuri yaMuungano wa Tanzania;

    (ii) Maoni ya Mabaraza ya Katiba kuhusu Rasimu ya Katiba ya Jamhuriya Muungano wa Tanzania;

    (iii) Maoni ya Wananchi kuhusu Sera, Sheria na Utekelezaji;(iv) Takwimu za Ukusanyaji wa maoni ya Wananchi kuhusu Mabadiliko

    ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;

    (v) Utafiti kuhusu Mabadiliko ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano waTanzania;

    (vi) Viambatisho vya Ripoti ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba; na(vii) Rasimu ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

    Mheshimiwa Rais,

    Kabla ya kukabidhi Ripoti yetu naomba univumilie niweze kusema

    machache lakini kwa maneno mengi. Napenda kuanza na shukrani. Baada

    ya kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutuwezesha kukamilisha kazi hii,

    shukrani zetu kwanza ni kwako Mheshimiwa Rais na Mheshimiwa Rais wa

  • 8/13/2019 Hotuba Ya Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba Mhe Joseph S. Warioba, Ripoti ya Tume kwa Rais Kikwet

    4/23

    4

    Zanzibar. Tunawashukuru kwa kututeua na pia kwa msaada mkubwa

    mliotupa. Kila tulipokwama mahali mlikuwa wepesi kutoa maagizo

    yaliyotukwamua. Tunawashukuru sana Mawaziri wa Katiba na Sheria,

    Wanasheria Wakuu wa Serikali, Makatibu Wakuu Viongozi na Watendaji

    Wakuu wa Wizara za Katiba na Sheria, Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa

    Wilaya, Wakurungenzi na Makatibu wa Mamlaka za Serikali za Mitaa,

    Watendaji wa Tarafa, Kata na Shehia, Vijiji na Wenyeviti wa Serikali za

    vijiji kwa ushirikiano mzuri walioutoa kwa Tume. Aidha, Tume inatoa

    shukrani za dhati kwa Jeshi la Polisi na Kamati za Ulinzi na Usalama za

    Wilaya kwa kuhakikisha mchakato mzima unakamilika kwa usalama.

    Tume pia inatoa shukrani kwa Vyama vya siasa, Jumuiya za Dini,

    Asasi za Kiraia, Taasisi na makundi mengine kwa mchango wao. Kwa

    namna ya pekee, tunavishukuru vyombo vya habari ambavyo, licha ya

    kusambaza taarifa mbalimbali zilizokuwa zikitolewa na Tume,

    vimeuelimisha Umma na kuufanya mchakato mzima wa katibakuwa wa

    wazi na wenye hamasa.

    Mwisho kwa uzito wa pekee Tume inawashukuru wananchi, hasa

    wananchi wa kawaida, kwa mchango wao mkubwa wa mawazo na maoni.

    Hii ni mara ya kwanza katika nchi yetu kwa wananchi wa kawaida

    kushiriki katika kutoa maoni kuhusu aina ya Katiba wanayoitaka na

    wamefanya hivyo kwa wingi na kwa uzito mkubwa.

  • 8/13/2019 Hotuba Ya Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba Mhe Joseph S. Warioba, Ripoti ya Tume kwa Rais Kikwet

    5/23

    5

    Mheshimiwa Rais,

    Kama nilivyosema mapema, pamoja na Ripoti ya Tume kuhusu

    mchakato wa katiba ambayo tunakabidhi leo, tunakabidhi pia na Rasimu

    ya Katiba. Rasimu hiyo ni ndefu kuliko Rasimu ya awali. Rasimu ya awali

    ilikuwa na ibara 240. Rasimu ya sasa ina ibara 271. Ongezeko la ibara

    kwa kiwango kikubwa limetokana na Tume kuzingatia maoni ya Mabaraza

    ya Katiba. Muhtasari wa Rasimu uko kwenye Sura ya Kumi na Mbili ya

    Ripoti yetu. Kwa leo nitagusia mambo machache ambayo Tume imeona

    vyema tukatoa maelezo.

    Jambo la kwanza, ni ushiriki wa wananchi katika mchakato mzima

    wa kupata katiba mpya. Tume ilipoanza kulikuwa na wasiwasi kwamba

    ushiriki wa wananchi wa kawaida ungekuwa dhaifu kwa sababu iliaminika

    kwamba wananchi kwa ujumla wao hawana ujuzi wa katiba. Lakini Tume

    iligundua mapema kwamba wananchi wanajua mambo mengi ambayo ni

    msingi wa katiba yoyote ile.

    Sura tano za mwanzo za Rasimu ya Katiba zinatokana na mchango

    mkubwa kutoka kwa wananchi, hasa kuhusu Misingi ya Taifa, Tunu za

    Taifa, Maadili na Miiko ya Uongozi, Dira ya Taifa na Haki za binaadam.

    Wananchi pia wametoa maoni mazito kuhusu uongozi na utawala wa

    nchi, ikiwa ni pamoja na nafasi ya wawakilishi wao Bungeni.

  • 8/13/2019 Hotuba Ya Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba Mhe Joseph S. Warioba, Ripoti ya Tume kwa Rais Kikwet

    6/23

    6

    Hii ni mara ya kwanza kwa nchi yetu kuwashirikisha kwa ukamilifu

    wananchi katika kutunga katiba ya nchi yao. Nia ya mchakato huu ni

    kupata katiba inayokubalika na wananchi. Ili katiba ikubalike na wananchi

    ni jambo la msingi maoni yao yapewe uzito unaostahili. Nayasema haya

    kwa sababu tangu Rasimu ya kwanza itolewe maeneo yaliyopewa uzito

    na wananchi hayakupewa uzito katika mijadala ya viongozi, wasomi na

    vyombo vya habari.

    Mheshimiwa Rais,

    Utangulizi wa Katiba unaeleza kuwa Katiba ya Jamhuri ya

    Muungano wa Tanzania imetungwa na Wananchi wa Tanzania. Utangulizi

    unatoa taswira na picha halisi ya Jamhuri ya Muungano na watu wake,

    historia yao, matarajio yao, misingi ya taifa na masuala muhimu ambayo

    Wananchi wanataka kuyaendeleza katika jamii, kizazi hadi kizazi.

    Sura ya Kwanza inaelekeza kuendelea kuwepo kwa Jamhuri ya

    Muungano wa Tanzania. Yapo pia masharti kuhusu alama za Taifa na

    sikukuu za Taifa na Rasimu inatambua Lugha ya Kiswahili kuwa Lugha ya

    Taifa. Imeainisha pia tunu za Taifa ambazo ni Uhuru, Haki, Udugu,

    Amani, Usawa, Umoja na Mshikamano. Tunu za Taifa ndiyo msingi wa

    maadili na taratibu mbalimbali za kimaisha za jamii mbali mbaliambazo

    hurithishwa kizazi hadi kizazi.

  • 8/13/2019 Hotuba Ya Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba Mhe Joseph S. Warioba, Ripoti ya Tume kwa Rais Kikwet

    7/23

    7

    Mheshimiwa Rais,

    Dira ya Taifa ni eneo ambalo wananchi walilitolea maoni kwa wingi

    na kwa uzito. Sura ya Pili ya rasimu kuhusu malengo muhimu, misingi ya

    mwelekeo wa shughuli za Serikali na sera za kitaifa imejumuisha maoni

    mengi ya wananchi. Wakulima, wafugaji, wavuvi na makundi mengine

    wanataka kuwe na dira ya Taifa ambayo ndiyo itakuwa mwongozo mkuu

    utakaofuatwa na kuzingatiwa na uongozi, hasa Serikali na vyama vya

    siasa katika kutekeleza shughuli za kisiasa, kiuchumi, kijamii, kiutamaduni

    na kimazingira.

    Sura ya Tatu imependekeza masharti kuhusu Maadili na Miiko ya

    Uongozi na Utumishi wa Umma. Uongozi ni dhamana, na kiongozi wa

    Umma anatakiwa kutekeleza wajibu wake kwa kuheshimu Wananchi,

    kukuza hadhi ya Taifa na kukuza imani na heshima ya Utumishi wa Umma

    kwa Wananchi. Rasimu imeorodhesha miiko ya uongozi ikiwa ni pamoja

    na kupiga marufuku kiongozi wa Umma kutumia wadhifa, nafasi ya

    madaraka au cheo chake kwa manufaa yake binafsi, familia yake, ndugu,

    jamaa, marafiki au mtu yeyote aliye na uhusiano naye wa karibu.

    Mheshimiwa Rais,

    Sura ya Nne, inahusu Haki za Binadamu, Wajibu wa Raia na

    Mamlaka za Nchi. Wananchi wametoa maoni mengi kuhusu haki za

  • 8/13/2019 Hotuba Ya Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba Mhe Joseph S. Warioba, Ripoti ya Tume kwa Rais Kikwet

    8/23

    8

    binadamu na hasa katika suala la utekelezaji na usimamizi wa haki hizo.

    Kutokana na maoni ya Wananchi, Rasimu imeboresha haki za binadamu

    zilizomo katika Katiba ya sasa na kuongeza haki mpya za mtu binafsi na

    haki za makundi mbalimbali kama vile watoto, wanawake, wazee, vijana,

    makundi madogo katika jamii, watu wenye ulemavu, wafanyakazi, waajiri

    na haki ya kutafuta, kutoa na kusambaza habari. Aidha, Rasimu

    imeainisha wajibu wa raia ikiwa ni pamoja na kulinda na kutetea Katiba

    na Sheria za Nchi; kulipa kodi, kuheshimu haki, uhuru na maslahi ya watu

    wengine na kulinda na kutunza mazingira.

    Sura ya Tano inahusu Uraia wa Jamhuri ya Muungano. Uraia ni

    mmoja, nao ni wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Rasimu ya Katiba

    inapendekeza kutambuliwa kwa uraia wa kuzaliwa na kujiandikisha

    ambao ni wa nchi moja. Aidha, Rasimu inapendekeza kuwapa hadhi

    maalum watu wenye asili au nasaba ya Tanzania ambao wameacha kuwa

    raia wa Tanzania kwa kuchukua uraia wa nchi nyingine.

    Mheshimiwa Rais,

    Kuhusu Serikali ya Jamhuri ya Muungano, Rasimu ya Katiba

    imefafanua kwa kina na ufasaha juu ya Rais wa Jamhuri ya Muungano

    ambaye ni alama na taswira ya nchi na Watu wake. Yeye peke yake

    ndiye mwenye hadhi na heshima ya Mkuu wa Nchi, Amiri Jeshi Mkuu na

  • 8/13/2019 Hotuba Ya Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba Mhe Joseph S. Warioba, Ripoti ya Tume kwa Rais Kikwet

    9/23

    9

    Kiongozi wa Serikali. Kwa kuzingatia maoni ya Wananchi, madaraka ya

    Rais na hasa yale ya uteuzi yamepunguzwa kwa kuweka vyombo vya

    kupendekeza majina ya Watu wa kuteuliwa na kwa baadhi ya vyeo

    kuhitaji kuthibitishwa na Bunge.

    Mheshimiwa Rais,

    Wananchi wametaka Katiba itambue mamlaka na madaraka yao

    juu ya wawakilishi wao katika Bunge, na kama ilivyokuwa katika Rasimu

    ya Awali, inapendekezwa Wabunge wasiwe Mawaziri, kuwe na ukomo wa

    uwakilishi katika Bunge na wapiga kura wawe na madaraka ya

    kumwajibisha Mbunge hata kabla ya kumalizika kwa muhula wake na

    Spika na Naibu Spika wasitokane na Wabunge au kiongozi wa juu wa

    chama cha siasa.

    Kuhusu Mahakama ya Jamhuri ya Muungano, Sura ya Kumi imebaki

    na mapendekezo ya awali ya kuanzishwa kwa Mahakama ya Juu

    (Supreme Court) na kuendelea kuwepo kwa Mahakama ya Rufani. Aidha,

    inapendekezwa, kama ilivyo katika Katiba ya sasa, Mahakama Kuu ya

    Tanzania Bara (Tanganyika) na Mahakama Kuu ya Zanzibar, ziendelee

    kuwa na mamlaka sawa ya kusikiliza katika ngazi ya awali, mashauri ya

    madai na jinai yanayohusu sheria za Serikali ya Jamhuri ya Muungano

    katika maeneo yao ya utawala (concurrent jurisdiction).

  • 8/13/2019 Hotuba Ya Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba Mhe Joseph S. Warioba, Ripoti ya Tume kwa Rais Kikwet

    10/23

    10

    Mheshimiwa Rais,

    Tume kwa kuzingatia maoni ya Wananchi, tofauti na ilivyokuwa

    katika Rasimu ya Awali, sasa inapendekeza Msajili wa Vyama vya Siasa

    iwe ni taasisi inayojitegemea na siyo kuwa Sehemu ya Tume Huru ya

    Uchaguzi.

    Kuhusu ulinzi na usalama, Sura ya Kumi na Tano inatamka kuwa

    jukumu la ulinzi na usalama wa Jamhuri ya Muungano ni la kila raia.

    Kwa kuzingatia maoni ya Wananchi waliyoyatoa katika Mabaraza ya

    Katiba, Rasimu sasa inapendekeza kuwepo kwa Jeshi la Polisi moja na

    Idara ya Usalama wa Taifa moja katika Jamhuri ya Muungano wa

    Tanzania.

    Mheshimiwa Rais,

    Mabadiliko makubwa ya Katiba lazima yaendane na masharti

    yatokanayo na Masharti ya Mpito ambayo nayo ni sehemu ya Katiba.

    Masharti haya yanaweka utaratibu, mfumo wa kikatiba na kisheria kuhusu

    masuala ya kiutawala, uongozi wa nchi, sheria za nchi, nafasi za

    madaraka na namna mambo yote hayo yatakaavyokuwa na kuendeshwa.

    Sura ya Kumi na Saba inapendekeza Muda wa Mpito wa Miaka

    Minne, kuanzia tarehe ya kuanza kutumika kwa Katiba Mpya hadi tarehe

    31 Desemba, 2018. Katika kipindi hicho, sheria zilizopo hivi sasa

  • 8/13/2019 Hotuba Ya Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba Mhe Joseph S. Warioba, Ripoti ya Tume kwa Rais Kikwet

    11/23

    11

    zitaendelea kutumika hadi zitakapobadilishwa. Sheria zinazotumika

    Tanzania Bara zitakuwa za Tanganyika na sheria zinzotumika Tanzania

    Bara na Zanzibar zitakuwa Sheria za Jamhuri ya Muungano. Yapo pia

    mapendekezo kuhusu masuala ya kufanyiwa kazi katika Muda wa Mpito.

    Mambo haya ni pamoja na:-

    (i) Kutungwa kwa Katiba ya Tanganyika;(ii) Kurekebisha Katiba ya Zanzibar ya Mwaka 1984 ili kuwiana

    na masharti ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa

    Tanzania ya mwaka 2014;

    (iii) Mgawanyo wa rasilimali baina ya Serikali ya Jamhuri yaMuungano na Serikali za Nchi washirika;

    (iv) Kuundwa kwa Tume na Taasisi za Kikatiba zilizoainishwakwenye Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya

    Mwaka 2014 na kwa kuzingatia masharti ya Katiba hiyo;

    (v) Kufanya maandalizi na kuendesha Uchaguzi Mkuu waMwaka 2015 kwa kuzingatia masharti ya Katiba ya Jamhuri

    ya Muungano ya Mwaka 2014; na

    (vi) Kufanya maandalizi ya mambo yote muhimu kwa ajili yautekelezaji bora wa masharti ya kikatiba yaliyomo kwenye

    Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka

    2014.

  • 8/13/2019 Hotuba Ya Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba Mhe Joseph S. Warioba, Ripoti ya Tume kwa Rais Kikwet

    12/23

    12

    Mheshimiwa Rais,

    Moja ya mambo ambayo yamejadiliwa sana na kwa hisia kali tangu

    Rasimu ya awali ilipotolewa na Tume ni Muungano wa Tanzania. Jambo

    kubwa limekuwa juu ya muundo wa Muungano. Wakati Tume inazindua

    Rasimu ya Awali tulisema hatukupendekeza kuendelea kuwa na muundo

    wa Serikali mbili kwa sababu mbalimbali. Tulisema kuwa kuendelea kwa

    Serikali mbili kulihitaji ukarabati mkubwa ambao tulifikiri hautawezekana.

    Mabaraza ya Katiba yalitoa maoni mengi ambayo yaliilazimu Tume

    kufanya tena uchambuzi wa kina. Kama ilivyokuwa katika Rasimu ya

    Awali, suala la muundo wa Muungano ndilo lililochukuwa muda mwingi

    wa Tume. Sheria ya Mabadiliko ya Katiba ilielekeza kwamba Tume

    itaongozwa na misingi mikuu ya kitaifa na maadili ya jamii ya kuhifadhi na

    kudumisha mambo kadhaa. Moja ya mambo hayo ilikuwa ni kuwepo kwa

    Jamhuri ya Muungano. Hivyo, Tume ilianza kazi kwa madhumuni ya

    kupata maoni ya kuboresha Muungano. Wananchi wengi walitoa maoni

    kuhusu Muungano, lakini wengi wao walijikita kwenye Muundo wake.

    Kwa Tanzania Bara, wananchi zaidi ya 39,000 walitoa maoni kuhusu

    Muungano na kati ya hao, karibu 27,000 walizungumzia muundo. Kwa

    Zanzibar, wananchi karibu wote waliotoa maoni walijikita kwenye suala la

    Muungano. Kati ya wananchi karibu 38,000 waliotoa maoni Wananchi

    19,000 walitoa maoni kuhusu muundo wa Muungano.

  • 8/13/2019 Hotuba Ya Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba Mhe Joseph S. Warioba, Ripoti ya Tume kwa Rais Kikwet

    13/23

    13

    Mchanganuo wa takwimu hizi unaonyesha kuwa kwa upande wa

    Tanzania Bara, 13% walipendelea Serikali moja, 24% walipendekeza

    Serikali mbili na 61% walipendekeza Serikali tatu. Kwa upande wa

    Zanzibar, 34% walipendekeza Serikali mbili na 60% walipendekeza

    Muungano wa Mkataba, na 0.1% (watu 25) walipendekeza Serikali moja.

    Aidha, taasisi nyingi kama vile vyama vya siasa, asasi za kiraia na jumuia

    za kidini zilipendekeza muundo wa Serikali tatu. Baadhi ya taasisi za

    kiserikali, ama moja kwa moja au kwa tafsiri ya mapendekezo yao, pia

    zilipendekeza Serikali tatu. Kwa mfano, Baraza la Wawakilishi Zanzibar

    lilipendekeza kuwepo kwa mamlaka huru ya Zanzibar, mamlaka huru ya

    Tanganyika na mamlaka ya Muungano na iwekwe wazi maeneo, uwezo,

    nguvu, utendaji na mipaka ya kila mamlaka. Ofisi ya Waziri Mkuu

    imependekeza mfumo wa serikali tatu ili kuondoa kero za muungano.

    Aidha, Mamlaka ya Mapato Tanzania imependekeza kuwepo kwa Serikali

    tatu ili kutoa majibu ya kero zilizopo na kuleta utulivu zaidi ilimradi

    upangiliwe vizuri.

    Mheshimiwa Rais;

    Baada ya kuona takwimu hizi na kuchanganua sababu zilizotolewa

    na makundi mbali mbali, Tume iliamua kufanya utafiti kuhusu muundo wa

    Muungano. Suala hili lilijitokeza kwa nguvu na hisia kali mara ya kwanza

    mwaka 1984 katika kipindi kilichoitwa kuchafuka kwa hali ya hewa

  • 8/13/2019 Hotuba Ya Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba Mhe Joseph S. Warioba, Ripoti ya Tume kwa Rais Kikwet

    14/23

    14

    kisiasa Zanzibar. Mwaka 1991 Tume ya Nyalali ilipendekeza Muundo wa

    Serikali tatu. Miaka miwili baadaye, yaani Mwaka 1993, kikundi cha

    Wabunge wa Tanzania Bara katika Bunge la Muungano, G55,

    kilipendekeza kuwa na muundo wa Serikali tatu na Bunge likaridhia.

    Mwaka 1999 Kamati ya Kisanga ilipendekeza muundo wa Serikali tatu.

    Tume pia imepitia taarifa ya Kamati nyingi zilizoundwa na Serikali ya

    Jamhuri ya Muungano na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, kama vile,

    Kamati ya Amina Salum Ali na Kamati ya Shelukindo ya mwaka 1994.

    Sababu zilizotolewa katika matukio hayo ya mwanzo kwa kiwango

    kikubwa, zinafanana na zile ambazo zimetolewa kipindi hiki. Kila upande

    wa Muungano una malalamiko mengi kuhusu muundo wa Muungano.

    Katika Taarifa ya Tume tunayokukabidhi leo, tumeorodhesha malalamiko

    kumi kwa upande wa Zanzibar na malalamiko manane kwa upande wa

    Tanzania Bara. Kwa upande wa Zanzibar malalamiko matatu makubwa

    ni;

    (i) Serikali ya Tanganyika imevaa koti la Serikali ya Muunganoambalo linaisaidia Tanganyika zaidi kuliko Zanzibar. Koti hilo

    limeifanya Tanganyika kuwa ndiyo Tanzania;

    (ii) Mambo ya Muungano yamekuwa yakiongezeka na hivyokuathiri madaraka ya Zanzibar (autonomy) na kufifisha hadhi

    ya Zanzibar (identity) na Zanzibar inaendelea kumezwa; na

  • 8/13/2019 Hotuba Ya Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba Mhe Joseph S. Warioba, Ripoti ya Tume kwa Rais Kikwet

    15/23

    15

    (iii) Kumwondoa Rais wa Zanzibar kuwa Makamu wa Rais waJamhuri ya Muungano.

    Kwa upande wa Tanzania Bara, malalamiko makubwa ni;

    (i) Zanzibar imekuwa nchi huru, ina bendera yake, ina wimbowake wa Taifa ina Serikali yake na imebadili Katiba yake ili

    ijitambue kama nchi, wakati Tanzania Bara imepoteza

    utambulisho wake. Katiba ya Jamhuri inasema Tanzania ni

    nchi moja lakini Katiba ya Zanzibar inasema ni nchi mbili;

    (ii) Zanzibar imebadili Katiba yake na kuchukua madaraka yaJamhuri ya Muungano, kama vile kuelekeza sheria za

    Muungano zilizopitishwa na Bunge la Muungano zipelekwe

    kwenye Baraza la Wawakilishi. Maana yake ni kuwa Katiba ya

    Zanzibar sasa ipo juu ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano; na

    (iii) Wananchi wa Tanzania Bara kutokuwa na haki ya kumilikiardhi Zanzibar wakati wenzao wa Zanzibar wana haki hiyo

    Tanzania Bara.

    Mheshimiwa Rais;

    Katika kuchambua malalamiko ya Zanzibar kwamba Tanganyika

    imevaa koti la Muungano, Tume imebaini kwamba muundo wa Muungano

    wa Serikali mbili umeifanya Serikali ya Muungano kwa kiwango kikubwa

  • 8/13/2019 Hotuba Ya Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba Mhe Joseph S. Warioba, Ripoti ya Tume kwa Rais Kikwet

    16/23

    16

    kushughulikia zaidi mambo ya Tanzania Bara, hasa mambo ya

    maendeleo. Kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano ya mwaka

    1977, Serikali ya Muungano ina mamlaka ya kusimamia mambo ya

    muungano na mambo yasiyo ya muungano kwa upande wa Tanzania

    Bara. Kwa msingi huo, Serikali ya Muungano inashughulikia sana mambo

    ya kilimo, elimu, afya, maji, nishati na madini, ujenzi, uchukuzi, maliasili

    na utalii na mengine ya Tanzania Bara ambayo siyo mambo ya

    Muungano. Wakati wa kikao cha Bajeti Bunge la Muungano hutenga siku

    mbili au tatu za majadiliano kwa Wizara zinazosimamia mambo haya

    yasiyo ya Muungano ya Tanzania Bara wakati mambo ya Muungano kama

    vile ulinzi, mambo ya nje na mambo ya ndani hutengewa siku moja au

    nusu siku. Maswali ya Wabunge kuhusu mambo ya maendeleo pia

    yanahusu Tanzania Bara na ziara za Wabunge kukagua miradi ya

    maendeleo zinahusu Tanzania Bara katika mambo yasiyo ya Muungano.

    Mambo haya Bungeni yanasimamiwa na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya

    Muungano ambaye, kihalisia hana mamlaka wala madaraka yoyote

    kuhusu Zanzibar.

    Aidha, muundo huu wa muungano pia umesababisha kuwepo kwa

    wizara au taasisi zenye sura au zinazotekeleza mambo ya muungano

    pekee; mambo ya Tanzania Bara na mambo mchanganyiko; kwa maana

    ya mambo ya muungano na mambo yasiyo ya muungano, hali ambayo

  • 8/13/2019 Hotuba Ya Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba Mhe Joseph S. Warioba, Ripoti ya Tume kwa Rais Kikwet

    17/23

    17

    inapekea ugumu wa kutofautisha gharama za muungano na zisizo za

    muungano katika wizara au taasisi hizo. Kundi la pili na la tatu ndio

    imekuwa chanzo cha kero za muungano.

    Hakuna njia ya kubadili hali hii kwa sababu Serikali ya Muungano

    haina mamlaka ya kutoshajuu ya mambo ya maendeleo kwa upande wa

    Zanzibar. Mawaziri wengi na Serikali kwa ujumla inalazimika kupanga

    maendeleo na kutafuta rasilimali kwa ajili ya Tanzania Bara zaidi kuliko

    kwa Zanzibar. Zanzibar hufanya mipango yake ya maendeleo. Lakini, ili

    kupata rasilimali kama mikopo na misaada ni lazima ipitie Serikali ya

    Muungano, jambo ambalo utekelezaji wake umesababisha matatizo

    mengi. Utatuzi wa matatizo hayo umekuwa mgumu, umechukua muda

    mrefu au umeshindikana. Njia pekee ambayo ingefanya maendeleo ya

    Zanzibar yapewe uzito sawa na mambo ya Tanzania Bara ni kuyaweka

    mambo hayo chini ya Serikali ya Muungano, yaani kuwa na Serikali moja.

    Hata hivyo, hilo likifanyika kuna hofu ya Zanzibar kumezwa.

    Mheshimiwa Rais;

    Tume imefanya uchambuzi wa ndani kuhusu malalamiko ya

    Zanzibar kwamba kuongezeka kwa Mambo ya Muungano kumeathiri

    madaraka ya Zanzibar (autonomy). Tangu mwanzo wa Muungano,

    ilikubalika kwamba Zanzibar ibaki na hadhi yake na iwe na madaraka

  • 8/13/2019 Hotuba Ya Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba Mhe Joseph S. Warioba, Ripoti ya Tume kwa Rais Kikwet

    18/23

    18

    kuhusu Mambo yasiyo ya Muungano. Tume ilifanya uchambuzi wa Mambo

    ya Muungano ili kubaini kama yanaingilia hadhi na uhuru wa Zanzibar.

    Kati ya Mambo 22 ya Muungano, Tume imebaini kuwa siyo mambo yote

    yanatekelezwa kikamilifu kimuungano. Mambo mengi yamebadilishwa bila

    ya kubadili katiba, ama kwa makubaliano kati ya pande zote mbili za

    Muungano au kwa hatua zilizochukuliwa na upande mmoja. Mambo hayo

    ni pamoja na kodi, bandari, leseni za viwanda, usafiri na usafirishaji wa

    anga, utafiti, posta na simu, uraia, takwimu, mafuta na gesi na

    Mahakama ya Rufani.

    Kwa hali halisi ilionekana hakuna uwezekano kuyarudisha kwenye

    orodha ya muungano mambo ambayo yameondolewa kiutekelezaji.

    Kwa kipindi cha miaka ishirini iliyopita, Kamati nyingi zimeundwa na

    kutoa mapendekezo ya kuondoa mambo mengi zaidi kutoka kwenye

    Orodha ya Mambo ya Muungano, ikiwa ni pamoja na elimu ya juu,

    biashara ya nje, uhusiano wa kimataifa, mikopo, misaada ya nje na

    mafuta na gesi. Wakati Tume inakusanya maoni, Wananchi wengi wa

    Zanzibar kutoka makundi mawili makubwa, yaani wale waliotaka

    Muungano wa Serikali Mbili na wale waliotaka Muungano wa mkataba,

    wote walipendekeza mambo hayo yaondolewe kwenye Orodha ya Mambo

    ya Muungano.

  • 8/13/2019 Hotuba Ya Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba Mhe Joseph S. Warioba, Ripoti ya Tume kwa Rais Kikwet

    19/23

    19

    Kwa tathmini ya Tume baadhi ya mambo haya hakuna budi

    yaondolewe kutoka orodha ya muungano la sivyo kero za muungano

    zitaendelea. Kwa mfano suala la uhusiano wa kimataifa likiendelea kuwa

    ni jambo la muungano Zanzibar haitaweza kujiunga na mashirika kama

    OIC na FIFA. Kwa msingi huo, Tume imependekeza kuliondoa suala la

    uhusiano wa kimataifa katika mambo ya muungano na kubakisha suala la

    mambo ya nje.

    Eneo jingine ni mgongano kati ya Katiba ya Muungano, na Katiba ya

    Zanzibar. Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 imeweka masharti kwamba

    sheria zinazotungwa na Bunge la Jamhuri ya Muungano hazitatumika

    Zanzibar hadi zipelekwe kwenye Baraza la Wawakilishi. Aidha, kodi

    itakayoamuliwa na Bunge kutozwa na Serikali ya Muungano lazima ipate

    ridhaa ya Baraza la Wawakilishi Zanzibar.

    Mambo haya yameleta mgongano wa Katiba. Juhudi zilizofanywa

    na pande zote mbili hazikufanikiwa kuondoa mgongano huo. Zaidi ya

    hapo, mabadiliko ya Katiba ya Zanzibar yaliyofanywa mwaka 2010

    yametamka wazi kwamba Zanzibar ni nchi kati ya nchi mbili za Muungano

    wakati Katiba ya Jamhuri inaelekeza kwamba Tanzania ni Nchi moja.

    Mabadiliko katika Katiba ya Zanzibar pia yamehamisha baadhi ya

    madaraka ya Serikali ya Muungano kwenda Zanzibar.

  • 8/13/2019 Hotuba Ya Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba Mhe Joseph S. Warioba, Ripoti ya Tume kwa Rais Kikwet

    20/23

    20

    Wakati wa kukusanya maoni ya wananchi, Tume ilibaini kwamba

    haitakuwa rahisi kubadili Katiba ya Zanzibar kuifanya Zanzibar kuonekana

    kuwa sehemu ya Jamhuri ya Muungano badala ya kuwa sura ya nchi

    kamili. Mabadiliko ya aina hiyo yatahitaji kura ya maoni kama Katiba ya

    Zanzibar inavyoelekeza. Kwa tathmini ya Tume, baada ya kuwasikiliza

    wananchi wa Zanzibar, ni dhahiri kwamba pendekezo la kuifanya Zanzibar

    isionekane kama nchi halitakubalika kwenye kura ya maoni.

    Kwa kifupi tathimini yetu ni kwamba ukarabati mkubwa unahitajika

    ili kuendelea na muundo wa Serikali mbili. Maeneo mawili makubwa

    yanahitaji mabadiliko. Jambo la kwanza ni kuwa na mambo ya kutosha

    kwenye orodha ya muungano, ikiwa ni pamoja na mambo ya maendeleo

    na kiuchumi. Jambo hilo likifanyika, litazidisha malalamiko kwa upande

    wa Zanzibar kuwa hadhi na madaraka yake yanazidi kupotea. Aidha,

    Mambo ya muungano yakipunguzwa sana Serikali ya Muungano itakuwa

    inashughulika zaidi na zaidi na mambo ya Tanganyika; na Zanzibar itaona

    Tanganyika ndiyo muungano. Lakini kwaupande mwingine, Tanganyika

    nayo itaona si haki nayo isiwe na uhuru wa kuendesha mambo yake kama

    ilivyo kwa Zanzibar.

    Jambo la pili ni kuondoa mgongano na mgogoro wa Katiba. Hiyo

    maana yake ni Zanzibar kubadili Katiba yake ili Zanzibar na Tanganyika

    ziwe ni sehemu za nchi moja badala ya kuwa nchi kamili. Kama Zanzibar

  • 8/13/2019 Hotuba Ya Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba Mhe Joseph S. Warioba, Ripoti ya Tume kwa Rais Kikwet

    21/23

  • 8/13/2019 Hotuba Ya Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba Mhe Joseph S. Warioba, Ripoti ya Tume kwa Rais Kikwet

    22/23

    22

    Pili ni Serikali ya Muungano kuwa na uhakika wa mapato kwa ajili ya

    kulipia gharama za Muungano. Tume imependekeza ushuru wa bidhaa

    uwe ni kodi ya Muungano. Kodi hii itakidhi sehemu kubwa ya matumizi

    ya Muungano na sehemu itakayobaki itapatikana kutokana na mapato

    yasiyo ya kodi yanayotokana na mambo ya muungano, michango ya Nchi

    Washirika na mikopo. Tatu ni kuundwa kwa Tume ya Uhusiano na

    Uratibu wa Serikali chini ya Uenyekiti wa Makamu wa Rais wa Muungano

    na itajumuisha viongozi wakuu wa nchi washirika. Majukumu ya Tume

    hiyo ni kusimamia mashauriano na mashirikiano kati ya Serikali ya

    Muungano na Serikali za nchi washirika ili kuhakikisha sera zinawiana na

    pia kusimamia na kuimarisha masuala yenye maslahi kwa taifa na pia

    kutatua migogoro.

    Mheshimiwa Rais;

    Kazi hii haikuwa rahisi hata kidogo. Sisi wajumbe kila mmoja

    tulikuwa tumetoka kwenye makundi tofauti tofauti. Kila mmoja wetu

    alikuwa na imani yake, maono yake, itikadi yake, msimamo wake na

    kadhalika. Lakini tulikubaliana mapema kabisa kwamba wajibu wetu ni

    kwa taifa. Kwa hivyo, tuliacha imani na misimamo yetu binafsi na

    kuamua kuwasikiliza wananchi kwa makini sana. Majadiliano yetu

    yalilenga kupata mwafaka wa kitaifa. Matokeo yake ni maamuzi ya

    maridhiano.

  • 8/13/2019 Hotuba Ya Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba Mhe Joseph S. Warioba, Ripoti ya Tume kwa Rais Kikwet

    23/23

    23

    Baadhi ya mapendekezo yetu kwa hakika yatapokelewa kwa

    hamasa kubwa. Lakini la muhimu ni kupata mwafaka wa kitaifa badala

    ya kufikia uamuzi kwa kujipima katika makundi.

    Baada ya kusema hayo machache lakini kwa maneno mengi, kwa

    heshima kubwa, naomba sasa kwa niaba ya Tume, kama sheria

    inavyoelekeza, nikukabidhi wewe Mheshimiwa Rais na Mheshimiwa Rais

    wa Zanzibar, Ripoti ya Tume pamoja na Viambatanisho vyake Saba,

    ikiwemo Rasimu ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.