jamhuri ya muungano wa tanzania2016/06/21  · 1 a. utangulizi 1. mheshimiwa spika, napenda kutumia...

37
JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA WIZARA YA FEDHA NA MIPANGO UFAFANUZI WA HOJA ZA WAHESHIMIWA WABUNGE AKICHANGIA HOTUBA ZA WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO MHE. DKT. PHILIP I. MPANGO (MB) AKIWASILISHA BUNGENI TAARIFA YA HALI YA UCHUMI 2015 NA MPANGO WA MAENDELEO WA TAIFA 2016/17 PAMOJA NA BAJETI KUU YA SERIKALI KWA MWAKA 2016/17 JUNI 20, 2016 DODOMA

Upload: others

Post on 30-Jan-2021

6 views

Category:

Documents


0 download

TRANSCRIPT

  • JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA

    WIZARA YA FEDHA NA MIPANGO

    UFAFANUZI WA HOJA ZA WAHESHIMIWA

    WABUNGE AKICHANGIA HOTUBA ZA WAZIRI WA

    FEDHA NA MIPANGO MHE. DKT. PHILIP I. MPANGO (MB)

    AKIWASILISHA BUNGENI TAARIFA YA HALI YA UCHUMI 2015 NA

    MPANGO WA MAENDELEO WA TAIFA 2016/17 PAMOJA NA BAJETI

    KUU YA SERIKALI KWA MWAKA 2016/17

    JUNI 20, 2016

    DODOMA

  • 1

    A. UTANGULIZI

    1. Mheshimiwa Spika, napenda kutumia fursa hii kukushukuru wewe

    binafsi, Naibu Spika na Wenyeviti wa Bunge kwa kuendesha vizuri

    majadiliano kuhusu Taarifa ya Hali ya Uchumi wa Taifa 2015 na Mpango

    wa Maendeleo wa 2016/17 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi

    ya Serikali kwa Mwaka 2016/17, niliyowasilisha tarehe 8 Juni, 2016.

    2. Mheshimiwa Spika, Kipekee, ninampongeza sana Mhe. Naibu

    Spika kwa umahiri na weledi wa hali ya juu alioonesha katika kusimamia

    Kanuni za Bunge wakati wote wa kikao hiki cha Bunge la bajeti. Hakika

    viwango vyake ni vya kimataifa. Japokuwa Mhe. Joseph Kakunda,

    mwanafunzi wangu Idara ya Uchumi Chuo Kikuu cha Dar-es-Salaam

    alichomekea sehemu fulani akidai kwamba mimi ni bahiri, (nadhani

    alimaanisha bahiri wa kutoa maksi za upendeleo!), nataka niliambie

    Bunge lako tukufu kwamba kwa viwango ambavyo Mhe. Naibu Spika

    alivyoonesha humu ndani, hakika ningempa maksi za haki asilimia 100

    kama walivyofanya maprofesa wake wa sheria UD na UCT. Hongera sana.

    3. Mheshimiwa Spika, napenda kutambua michango iliyotolewa na:

    Kamati ya Bajeti, chini ya M/kiti wake Mheshimiwa Hawa Abdulrahman

    Ghasia, Mbunge wa Mtwara Vijijini; Mheshimiwa David Ernest Silinde,

    Mbunge wa Momba, Naibu Msemaji Mkuu wa Kambi Rasmi ya Upinzani

    Bungeni kuhusu Wizara ya Fedha na Mipango, na waheshimiwa Wabunge

    wote waliochangia kwa kuzungumza au kwa maandishi hapa Bungeni.

    Ninawashukuru wote.

  • 2

    4. Mheshimiwa Spika, jumla ya Wabunge 158 wamechangia hoja

    niliyowasilisha. Kati ya hao, 133 wamechangia kwa kuzungumza na 25

    kwa maandishi.

    B: HATUA ZILIZOPONGEZWA NA WABUNGE WENGI

    5. Mheshimiwa Spika, Hatua zilizopongezwa na Wabunge wengi

    wakati wa mjadala juu ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa na Bajeti ya

    Serikali 2016/17 ni pamoja na zifuatazo:

    Kuthubutu kutenga asilimia 40 ya bajeti yote kwa ajili ya

    kutekeleza miradi ya maendeleo, ikiwa pamoja na kuanza ujenzi

    wa reli mpya ya kati kwa kiwango cha standard gauge, barabara,

    umeme, ununuzi wa meli mpya ziwa Victoria na ndege tatu za

    abiria;

    Kuongeza ukusanyaji wa kodi na mapato yasiyo ya kodi hadi

    kufikia wastani wa shilingi 1.2 trilioni kwa mwezi kwa kuziba

    mianya ya uvujaji wa mapato na kuimarisha matumizi ya vifaa vya

    kielektroniki (EFDs) katika ukusanyaji wa mapato, na Hazina kutoa

    fedha hizo kama ilivyopangwa;

    Kusimamia nidhamu ya matumizi na kupunguza matumizi yasiyo

    ya lazima ikiwa pamoja na safari za nje, posho, sherehe, kuondoa

    watumishi hewa katika utumishi wa umma;

    Kuhimiza azma ya kufanya kazi na kurejesha nidhamu ya

    watumishi kazini kwa ajili ya maendeleo ya Taifa;

  • 3

    Kuwapunguzia wafanyakazi mzigo wa PAYE na SDL kwa waajiri;

    Kuanzisha mahakama ya kushughulikia mafisadi;

    Kuweka kipaumbele katika kufufua na kujenga viwanda ili

    kupanua fursa za ajira na wigo wa kodi; na

    Kujielekeza kutekeleza Ilani ya CCM 2015, ahadi za viongozi

    wakuu na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025 ili kutatua kero za

    wananchi, hasa masikini.

    C: USHAURI ULIOTOLEWA NA WABUNGE WENGI

    6. Mheshimiwa Spika, Wabunge wengi pia walitoa ushauri katika

    maeneo mbalimbali, ili yazingatiwe katika bajeti hii au bajeti zijazo.

    Naomba kurejea ushauri muhimu uliotolewa na Wabunge kama

    ifuatavyo:

    Kuongeza tozo kwenye mafuta ili mapato hayo yatumike kupanua

    huduma za maji na na kukamilisha vituo vya afya na zahanati

    vijijini;

    Kuboresha mfumo wa kodi ikiwa pamoja na kufuta kodi, ushuru

    na tozo za kero kwa wakulima, wafugaji, wavuvi, wafanyabiashara

    wadogo, wakati na wakubwa/ wawekezaji, lakini pia kutoa ahueni

    ya kodi kwenye taulo za akinamama na vifaa vya watu wenye

    ulemavu, vifaa vya michezo, zana za uvuvi, na kulinda viwanda

    vya ndani;

  • 4

    Kuchukua hatua za ziada kuimarisha sekta ya kilimo, mifugo na

    uvuvi kwa kuongeza kilimo cha umwagiliaji, pembejeo, ugani,

    utafiti, mnyororo wa thamani, masoko, ruzuku, mikopo na bajeti

    ya kilimo;

    Kuimarisha utalii kwa kuzingatia fursa za kipekee za Tanzania

    katika sekta hii;

    Kuchukua hatua madhubuti kulinda mazingira na kukabiliana na

    athari za mabadiliko ya tabianchi;

    Shilingi milioni 50 zilizoahidiwa kwa kila kijiji ziwekewe utaratibu

    mzuri na endelevu;

    Kuongeza kasi ya kulipa madeni ya ndani (watumishi, wastaafu,

    wakulima, watoa huduma & makandarasi);

    Kuimarisha elimu na kuhakikisha inaendana na mahitaji ya

    wataalam wa Tanzania ya leo na kesho;

    Kupanua wigo wa kodi hususan katika sekta zenye mapato

    makubwa kama mawasiliano, madini, maliasili na ardhi, na sekta

    nyingine zenye fursa kama uvuvi na biashara kwenda nchi jirani,

    e-commerce, gawio kutoka katika mashirika ya umma, sambamba

    na kuhakikisha kila mwananchi analipa kodi stahiki ili kuchangia

    maendeleo ya Taifa na kupunguza utegemezi;

  • 5

    Kupambana na uvujaji wa mapato hususan katika biashara ya

    mafuta, miamala ya kielektroniki, transfer pricing na misinvoicing,

    misamaha ya kodi, wizi na udanganyifu katika ukadiriaji wa kodi,

    maduka ya jumla, n.k.

    Kuimarisha ushirikishwaji wa wadau ikiwa ni pamoja na Bunge,

    katika maandalizi ya mipango na bajeti ya Serikali;

    Kuendeleza utulivu wa uchumi ikiwa pamoja na kudhibiti mfumuko

    wa bei, kuongezeka kwa kasi deni la Taifa, kushuka kwa thamani

    ya shilingi, matumizi ya dola sambamba na shilingi (dollarisation),

    kupanua huduma za kibenki hadi vijijini na kupunguza riba;

    Kuboresha sheria mbalimbali ili kuboresha mazingira ya uwekezaji

    na kufanya biashara nchini;

    Kuchukua tahadhari katika kufanya mageuzi katika mfumo wa kodi

    na tozo nchini ili kuepuka kudhoofisha halmashauri na utekelezaji

    wa dhana ya (ugatuaji madaraka D by D);

    Kutoa msukumo zaidi kwa ushiriki wa sekta binafsi katika

    utekelezaji wa miradi ya kipaumbele, ikiwa pamoja na PPP;

    Kuanzisha duka la kununua madini kutoka kwa wafanya biashara

    wadogo kutoka nchi jirani na kutoza kodi ya asilimia moja

    Kuandaa mikakati mahsusi kwa ajili ya kukabiliana na umasikini

  • 6

    katika mikoa masikini zaidi ikiwa ni pamoja na kuangalia upya

    uwiano katika mgawanyo wa fedha na rasilimali nyingine za

    umma; na

    Kuongeza bajeti ya Ofisi ya Taifa ya Ukaguzi ili kuiwezesha

    kufanya kazi zake kwa ufanisi;

    D: UFAFANUZI WA BAADHI YA HOJA

    7. Mheshimiwa Spika, zipo hoja zilizotolewa na Kamati ya Bajeti, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni na kurudiwa na Waheshimiwa Wabunge

    wengi, ambazo baadhi yake napenda kuzitolea ufafanuzi kama ifuatavyo:

    Hoja Na. 1: Pendekezo la kuongeza Tozo ya shilingi 50 kwenye

    mafuta kwa ajili ya kutunisha Mfuko wa maji na kukamilisha

    ujenzi wa vituo vya afya na zahanati vijijini

    Ufafanuzi:

    Mheshimiwa Spika, hili ni pendekezo lenye lengo zuri na Serikali

    inalipokea. Hata hivyo, ni vema kutambua kwamba kufuatia

    kupungua kwa bei ya mafuta katika soko la dunia, gharama ya

    mafuta yote yaliyoagizwa kutoka nje imepungua (kwa takriban

    20%) na kuchangia kushuka kwa mfumuko wa bei (sasa umefikia

    5.2%). Mwenendo huu hakika umeleta ahueni kwa wananchi wetu

    wengi. Hivyo, kwa sasa Serikali imeamua kutoongeza tozo kwenye

    mafuta ili wananchi waendelee kunufaika na unafuu huo wa bei ya

    mafuta. Ni dhahiri kuwa ongezeko la tozo katika mafuta ya petroli

    na dizeli litasabisha kupanda kwa bei ya mafuta nchini jambo

  • 7

    ambalo litaongeza gharama za uzalishaji, usafirishaji na

    usambazaji wa chakula na bidhaa kama vifaa vya ujenzi na

    huduma nyingine.

    Aidha, wataalam wa uchumi wanashauri kuwa kipindi kama hiki

    cha uwepo wa bei ndogo ya mafuta ni fursa nzuri kwa nchi

    kuwekeza, hususan katika ujenzi wa miundombinu, viwanda

    (energy-intensive sectors) na kuendeleza ujuzi na teknolojia.

    Ndiyo sababu Serikali inaona kuwa ni busara Zaidi badala ya

    kuongeza tozo kwenye mafuta, tujielekeze kuongeza bajeti ya

    kutekeleza miradi mikubwa ya miundombinu ya usafirishaji, nishati

    na elimu sambamba na kutumia fedha zilizopangwa kwa ufanisi

    Zaidi.

    Hata hivyo, kwa kutambua umuhimu mkubwa wa kuboresha

    huduma ya maji nchini, ambayo ni ahadi ya muhimu katika Ilani

    ya CCM, bajeti ya maendeleo kwa Wizara ya Maji kwa mwaka wa

    fedha 2016/17 fedha za ndani zimeongezwa kwa asilimia 85

    kutoka shilingi bilioni 373.01 mwaka 2015/16 hadi Shilingi bilioni

    690.16 mwaka ujao wa fedha 2016/17. Kufuatia jitihada kubwa

    zinazoendelea kuongeza ukusanyaji wa mapato, Serikali

    itahakikisha fedha hizi zinapatikana na kutolewa kwa ajili ya

    utekelezaji wa miradi ya maji vijijini kama ilivyokusudiwa. Aidha,

    kwa upande wa haja ya kukamilisha ujenzi wa zahanati vijijini na

    vituo vya afya katika kata, Wizara ya afya inajipanga kufanya

    kwanza tathmini ya majengo hayo katika mwaka 2016/17 kwa ajili

    ya utekelezaji 2017/18.

  • 8

    Hoja Na. 2: Pendekezo la kuondoa msamaha wa kodi ya Mapato

    kwenye kiinua mgongo cha Waheshimiwa Wabunge.

    Ufafanuzi:

    Mheshimiwa Spika,

    Kwa mujibu wa Sheria ya Kodi ya Mapato, Sura 332 kodi ya

    mapato hutozwa kwenye vyanzo vyote vya mapato (global

    income);

    Kiinua mgongo ni chanzo kimojawapo cha mapato

    kinachotambuliwa na Sheria na hutozwa kodi;

    Kupitia Jedwali la Pili la Sheria ya Kodi ya Mapato, kiinua mgongo

    kinacholipwa kwa wabunge wakati wanamaliza muhula wa miaka

    mitano kimesamehewa kodi;

    Msamaha huu hauzingatii kanuni ya usawa ya utozwaji kodi, kwani

    watu wengine wote wanaopata malipo ya kiinua mgongo, iwe

    katika sekta binafsi au utumishi wa umma, hutozwa kodi katika

    mapato hayo. Kwa hiyo, hatua hii imechukuliwa ili kujenga misingi

    ya usawa na haki katika ulipaji wa kodi; na

    Lengo la kufanya marekebisho hayo sasa ni kwa ajili ya kuweka

    utaratibu wa kisheria ambao utatumika kukokotoa stahili za

    Mbunge endapo ukomo wa Mbunge yeyote utatokea katika kipindi

    cha kuanzia Julai, 2016 na kuendelea. Aidha, mabadiliko haya

  • 9

    yanafanyika sasa ili kuzingatia msingi wa utozaji kodi ambao

    inataka kodi iwe inatabirika (predictability principle).

    Mheshimiwa Spika, Naomba niliarifu Bunge lako Tukufu kwamba

    siku nilipowasilisha pendekezo hili kwa Mhe. Dkt. John Pombe

    Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,

    aliridhia mara moja na kusisitiza kwamba kulipa kodi ni wajibu wa

    Watanzania wote ili tujenge nchi yetu. Na kwa kuwa kiongozi

    lazima aongoze kwa mfano alielekeza kuwa yeye ni Mbunge wa

    Tanzania nzima na anapenda awe wa kwanza kukatwa kodi stahiki

    kwenye mafao yake ya kustaafu!

    Hivyo, napenda kufafanua kwamba marekebisho niliyowasilisha

    mbele ya Bunge lako Tukufu tarehe 8 Juni 2016 katika hotuba

    yangu ya Mapendekezo ya Serikali Kuhusu Makadirio ya Mapato

    na Matumizi ya Fedha kwa mwaka 2016/17 maana yake ni kuwa

    kiinua mgongo cha viongozi wote wa kisiasa waliotajwa

    kusamehewa kodi chini ya Sheria ya Mafao ya Viongozi wa kisiasa

    (The Political Service Retirement Benefits Act 1995) sasa kitakatwa

    kodi! Hivyo, kiinua mgongo cha Mhe. Samia Suluhu Hassan

    Makamu wa Rais, kitakatwa kodi! Mhe. Kassim M. Majaliwa, Waziri

    Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mbunge wa

    Ruangwa naye atakatwa kodi! Vivyo hivyo, Mhe. Spika na Naibu

    Spika watakatwa kodi! Aidha, Mawaziri (wakianza na Waziri wa

    Fedha) na Naibu Mawaziri wote sisi ni wabunge, hivyo kiinua

    mgongo chetu kitakatwa kodi! Wakuu wa Mikoa na Wilaya

    kadhalika kiinua mgongo chao kitakatwa kodi!! Mabadiliko haya ni

  • 10

    kwa mujibu wa kifungu 10(3) cha Sheria ya Kodi ya Mapato

    ambacho kimeweka sharti la kutotambua misamaha mingine

    yoyote ya kodi ya mapato ambayo haijatolewa kwa mujibu wa

    sheria hii.

    Hoja Na.3: Ofisi ya Taifa ya Ukaguzi (NAO) ametengewa fedha

    kidogo sana kuweza kutekeleza majukumu yake ipasavyo. Hivyo,

    bajeti ya ofisi hiyo iongezwe.

    Ufafanuzi:

    Mheshimiwa Spika,

    Ukomo wa bajeti ya matumizi mengineyo (OC) uliotengwa kwa

    mafungu mbalimbali umezingatia maamuzi na mkakati wa Serikali

    wa kupunguza matumizi ya kawaida na kuelekeza fedha nyingi

    katika bajeti ya miradi ya maendeleo;

    Katika kufikia ukomo wa matumizi mengineyo kwa Serikali nzima

    (Wizara, Idara, Taasisi za Kiserikali, Mikoa na Halmashauri)

    uchambuzi wa kina ulifanyika kubaini mahitaji ya fedha ambayo

    siyo ya lazima kwa wakati huu na hivyo hayawezi kuathiri utendaji

    wa taasisi husika. Miongoni mwa mahitaji yaliyopunguzwa ni:

    gharama za kumbi za mikutano, mafunzo na safari nje zisizo za

    lazima, maadhimisho na sherehe, posho na kudhibiti matumizi ya

    magari kwa mafungu yote. Aidha Serikali iliangalia miradi ambayo

    inaweza kutekelezwa kwa awamu;

  • 11

    Hata hivyo, Serikali inatambua umuhimu na majukumu ya msingi

    ya Ofisi ya Taifa ya Ukaguzi, kama ilivyo kwa taasisi nyingine

    nyeti, ikiwemo vyombo vya ulinzi na usalama, mihimili mingine ya

    Dola na uwezo wa kukabiliana na dharura. Hivyo, endapo

    kutajitokeza mahitaji ya lazima ambayo yatakwama kutekelezwa

    na ofisi ya CAG kutokana na ufinyu wa bajeti, Serikali itahakikisha

    mahitaji hayo yanazingatiwa wakati wa mapitio ya utekelezaji wa

    bajeti kwa kipindi cha nusu mwaka.

    Hoja Na.4: Ushuru wa bidhaa kutozwa kwenye ada ya miamala ya

    uhawilishaji wa fedha utaathiri mtumiaji wa mwisho na si

    makampuni ya simu

    Ufafanuzi:

    Mheshimiwa Spika,

    Ushuru wa bidhaa unaopendekezwa katika miamala ya fedha

    (Excise Duty on Money Transfer) hautakatwa kwenye fedha

    zinazotumwa au kupokelewa, bali katika ada inayotozwa na benki

    au kampuni ya simu;

    Kwa sasa Sheria inatamka kwamba ada hii itatozwa katika kutuma

    fedha tu. Hata hivyo, baadhi ya kampuni za simu na benki

    zimekuwa zikitumia mwanya wa Sheria hiyo kupunguza wigo wa

    kodi kwa kutoza ada wakati wa kupokea tu;

    Kwa mapendekezo haya, ushuru wa bidhaa utatozwa kwenye ada

    ya miamala ya uhawilishaji fedha ama wakati wa kutuma au

    kupokea fedha au vyote viwili kadri itakavyotozwa; na

  • 12

    Mantiki yake ni kuwa, ushuru huu utalipwa na benki au kampuni

    ya simu na siyo mtumaji au mpokeaji. Hata hivyo, Mamlaka ya

    Udhibiti wa Mawasiliano Tanzania (TCRA) kwa kushirikiana na

    Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na Benki Kuu ya Tanzania

    (BoT), itawajibika kuhakikisha kwamba tozo hiyo inaendana na

    uhalisia wa huduma itolewayo na kufanya ukaguzi (cyber forensic

    audit) wa miamala ya makampuni ya simu kabla na baada ya tozo

    ili yasihamishie mzigo kwa mtumiaji wa mwisho.

    Hoja Na. 5 Tathmini ya hali ya umasikini kimkoa

    Ufafanuzi:

    Mheshimiwa Spika,

    Viashiria vya kupima hali ya umaskini nchini hupatikana kwa

    kutumia Utafiti wa Mapato na Matumizi katika kaya ambao

    hufanyika kila baada ya miaka mitano hapa Nchini. Utafiti wa

    mwisho ulifanyika mwaka 2011/12.

    Mheshimiwa Spika,

    i. Hali ya umaskini katika kaya hupimwa kwa kuangalia mahitaji ya msingi (basic needs) kwa kila mwanakaya ukijumuisha mahitaji ya chakula yenye kiwango cha kilo kalori 2,200 kwa mlo kwa siku na hii ni kutokana na Kipimo cha Shirika la Afya Duniani - WHO. Mbinu hii inaonesha kiwango cha chini kabisa cha kipato anachohitaji mtu kwa ajili ya kukidhi mahitaji mbali mbali ya msingi.

    ii. Kiwango cha umaskini wa chakula hupimwa kwa gharama ya

    kiwango cha chini cha aina mbali mbali ya vyakula vyenye

  • 13

    kufikia kiwango cha kilo kalori 2,200 kinachohitajika kwa mlo wa mtu maskini kwa siku katika mwezi. Kwa utafiti huu gharama ya kununulia chakula cha mtu mmoja kwa siku bila kujali eneo alilotoka ni Shillingi 858. Kiwango cha umaskini wa chakula ni gharama ya matumizi yote ya kaya ambayo yapo chini ya gharama wanayohitaji ili kukidhi mahitaji ya chakula yaani (Food Poverty Line). Na kwa umaskini wa mahitaji ya msingi ambao huhusisha chakula ni Tshs. 1,216 (Basis Needs poverty line) kwa siku kwa kila mtu mmoja tu.

    Mheshimiwa Spika, utafiti wa kukusanya taarifa za kupima hali

    ya umasikini nchini hukusanya matumizi na mapato ya kaya.

    Taarifa zinazokusanywa ni umri, hali ya ndoa, elimu na afya,

    manunuzi na matumizi ya kaya, umiliki wa bidhaa za matumizi na

    mali, makazi na vifaa vya ujenzi, upatikanaji wa huduma na vifaa,

    shughuli za ajira na kiuchumi, utalii na shughuli za kilimo.

    Uchambuzi wa kina wa hali ya umaskini katika ngazi ya mkoa na

    wilaya yaani (Poverty Mapping) uliongozwa na wataalam wa

    REPOA na ulibainisha kuwa: Region Watu Wanaoishi Chini Mstari

    wa Umaskin 2000/01 (%)

    Watu Wanaoishi Chini

    Mstari wa Umaskini

    2011/12 (%)

    Mwanza 43 35

    Kagera 29 39

    Kigoma 38 49

    Singida 49 38

    Geita Included in Mwanza 44

  • 14

    Mheshimiwa Spika, sababu zinazoeleza kwanini kiwango cha

    umasikini katika Mikoa kama Mwanza, Kigoma, Singida, Geita, na

    Kagera ni kikubwa zaidi ukilinganisha na mikoa ya Lindi na Mtwara

    ni nyingi.

    Umasikini wa kipato ni mkubwa zaidi pale ambapo wananchi

    wengi zaidi wanaishi vijijini (33.3%) ikilinganishwa na mijini

    (21.7%). Mfano: Mwaka 2000/01 umaskini wa Kipato mkoa wa

    Mwanza ulikuwa 48%. Baada ya kugawanywa na kutolewa Wilaya

    ya Geita ambayo ilikuwa inaongoza kwa Umaskini wa Kipato

    62.3% na kuwa Mkoa mpya wa Geita kiwango cha umasikini Mkoa

    wa Mwanza kinaonekana kupungua kutoka 43% (2000/01) hadi

    35% (2011/12). Aidha, kwa mkoa wa Geita, sababu mojawapo ya

    umasikini wa kipato (44%) ni kiwango kikubwa cha uzazi (wastani

    wa watoto 7 kwa kila mwanamke mwenye umri wa kuzaa). Hivyo,

    shughuli za kiuchumi zinaelemewa na ongezeko kubwa la idadi ya

    watu (population explosion).

    Aidha, wilaya za Kwimba na Sengerema umaskini wa kipato ni

    39% na Misungwi 50% mwaka 2011/12. Wilaya za Mijini ambazo

    ni Nyamagana na Ilemela umaskini wa kipato ni 17% na 15%.

    Hivyo wananchi wengi vijijini kutegemea kilimo, ufugaji na uvuvi

    usio na tija, havitoshi kupunguza umaskini wa kipato kwa kasi

    inayotakiwa. Hivyo, zitahitajika jitihada za makusudi kuongeza tija

    katika shughuli za msingi za kiuchumi vijijini.

  • 15

    Mheshimiwa Spika, umasikini katika mkoa wa Kigoma

    unachangiwa na miundombinu hafifu ya usafirishaji ambao

    unapunguza fursa za masoko. Pia Kigoma inabeba mzigo mkubwa

    wa wakimbizi na hivyo kusababisha ziada inayozalishwa kutumika

    zaidi kulisha wakimbizi na kupunguza ustawi wa Kaya katika mkoa

    husika.

    Kwa mikoa ya Lindi na Mtwara umaskini huenda umepungua

    kutokana na kuongezeka kwa shughuli za biashara na uchumi

    kufuatia ugunduzi wa gesi asilia na ujenzi wa Kiwanda cha Saruji.

    Aidha, ongezeko la idadi ya watu kwa mwaka kwa mikoa hii ni chini

    ya wastani wa Taifa wa 2.7%. maana yake ni kuwa

    kinachozalishwa kinatumika katika kustawisha uchumi katika kaya

    zao.

    Mheshimiwa Spika, kwa mkoa wa Pwani, Wakazi wake wengi

    wanafanyia shughuli zao za kuongezea kipato katika Jiji la Dar es

    Salaam ambalo lina fursa nyingi Kiuchumi. Kadhalika, Pwani

    imepata fursa nyingi za Wakazi wake kujiongezea kipato chake

    kutokana na kuimarika kwa miundombinu ya barabara, maji na

    umeme ambazo ni vichecheo vya kuinua kipato cha Mwananchi

    mmoja mmoja.

  • 16

    Hoja Na. 6 Wizara ya Fedha na Mipango iangalie upya kuondoa

    misamaha ya kodi kwenye taasisi za dini kwa kuwa zinatoa

    huduma za kijamii kama shule, hospitali, n.k.

    Ufafanuzi:

    Mheshimiwa Spika,

    Baada ya kupokea maoni kutoka kwa wadau mbalimbali pamoja

    na waheshimiwa wabunge, utaratibu niliopendekeza kwa taasisi za

    kidini kulazimika kulipa kodi kwanza kwa bidhaa watakazonunua

    au kuagiza nje na kodi hiyo kurejeshwa baada ya ukaguzi

    kufanyika na kujiridhisha kuwa bidhaa hizo zimetumika kwa

    malengo yaliyokusudiwa umeonekana unaweza kukwamisha au

    kuchelewesha utekelezaji wa miradi inayotekelezwa na taasisi za

    kidini na kusababisha athari katika upatikanaji wa huduma

    muhimu kwa jamii. Kwa kutambua mchango mkubwa wa taasisi

    mbalimbali za kidini katika utoaji wa huduma za elimu na afya,

    napendekeza kufuta utaratibu niliotangaza katika hotuba ya bajeti

    na badala yake Serikali itaimarisha zaidi hatua mbalimbali za

    udhibiti wa misamaha ya kodi kama ifuatavyo:

    i. Taasisi za kidini kuwasilisha vifaa vinavyotarajiwa kununuliwa kutoka nje ya nchi kila mwanzo wa mwaka wa kalenda, na kuthibitisha kama vifaa vilivyopewa msamaha mwaka uliopita vilitumika kama sheria inavyotaka;

    ii. Kuwasilisha majina ya watu walioidhinishwa na Shirika au

    Taasisi kuandika barua za kuomba msamaha wa kodi, wakiainisha cheo, saini, picha, anwani na namba zao za simu.

  • 17

    Taarifa hizo ni muhimu katika kuiwezesha Mamlaka ya Mapato Tanzania kufuatilia bidhaa zilizoombewa na kupewa msamaha kama zimepata kibali cha taasisi hizo na zimetumika kutekeleza miradi iliyotarajiwa. Pia wanapaswa kuandika barua ya kumuidhinisha wakala wa forodha waliomteua kutoa mizigo itakayokuwa ikiagizwa kutoka nje;

    iii. Kila wanapoomba msamaha wanapaswa kupata barua kutoka

    kwa Afisa Mtendaji wa Serikali ya Mtaa na Mkuu wa Wilaya mahali Taasisi au Mradi unaotekelezwa ulipo ili kuthibitisha kuwepo kwa Taasisi au mradi na mahitaji ya vifaa vinavyoombewa msamaha;

    iv. Magari yanayoagizwa kwa msamaha yawe na namba na rangi

    maalum za utambuzi mfano: TEV 222 AXZ kama njia ya kudhibiti matumizi yake; na

    v. Taasisi ya dini itakayothibitika kutumia vibaya msamaha wa

    kodi itafutiwa usajili na Serikali.

    Mheshimiwa Spika, utaratibu na hatua mbalimbali za udhibiti

    wa misamaha ya kodi kwa wafanyabiashara, watumishi wa umma

    na taasisi zisizo za kiserikali utatangazwa katika gazeti la Serikali

    na kupitia vyombo vya habari.

  • 18

    Hoja Na.7: Uwezo wa TRA kukusanya Kodi ya Majengo

    Ufafanuzi

    Mheshimiwa Spika,

    TRA ni mamlaka ambayo ina uzoefu wa kutosha katika ukusanyaji

    kodi za Serikali na ina vituo vya ukusanyaji kodi katika Wilaya na

    Mikoa yote Tanzania;

    TRA inatekeleza majukumu yake kupitia sheria mbalimbali ambazo

    zinarahisisha ukusanyaji wa kodi kwa kupitia utaratibu wa kisasa

    wa Benki pamoja na njia za kielektroniki. Aidha, Kamishna Mkuu

    anaruhusiwa kama ataona inafaa, kuazima baadhi ya watumishi

    wenye uzoefu wa utozaji kodi ya majengo toka maeneo mengine

    ya serikali ikiwemo serikali za mitaa kwa lengo la kujenga

    ushirikiano na kuongeza ufanisi; na

    Kwa kutumia uzoefu na mifumo iliyopo ya TRA, ni wazi kuwa kodi

    ya majengo itakusanywa kwa ufanisi mkubwa na kwa uwazi zaidi,

    tofauti na sasa ambapo wananchi wengi hawalipi kodi hiyo.

    Kuhusu Viwango vya Kodi ya Majengo

    Waziri wa Fedha na Mipango ataweka viwango vya kodi ya

    majengo baada ya kushauriana na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais

    TAMISEMI ili kuweka uwazi na kujumuisha maoni ya wadau wote

    muhimu zikiwemo Halmashauri husika; na

    Kodi ya majengo itatozwa kwa kuzingatia mazingira ya maeneo

    husika ambapo TRA itakuwa na jukumu la kutoza, kukusanya na

  • 19

    kuwasilisha makusanyo hayo kwenye akaunti maalumu kwa

    manufaa ya serikali za mitaa.

    Mapato kutokana na kodi ya majengo yataingizwa katika mfuko

    mkuu. Mawaziri wenye dhamana ya Fedha na TAMISEMI

    watashauriana kuhusu mgawanyo wa fedha hizo kwa kuzingatia

    bajeti za Halmashauri husika.

    Hoja Na.8: Kutoza Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) katika

    Huduma za Utalii

    Ufafanuzi:

    Mheshimiwa Spika,

    Kabla ya hotuba ya bajeti ya 2016/17 nchi zote wanachama wa

    Jumuiya Afrika Mashariki zilikuwa zinatoza VAT kwenye huduma

    ya utalii isipokuwa Tanzania ambayo imependekeza kutoza katika

    bajeti yake ya mwaka 2016/17;

    Mwaka 2014 Serikali kupitia Bunge ilitunga sheria ya VAT. Sheria

    hii ilitungwa ili kutatua upungufu uliokuwepo katika sheria ya VAT

    ya mwaka 1997;

    Msamaha wa VAT kwenye huduma za utalii ulifutwa mwaka 2014

    baada ya kukubaliana na wadau ambao waliiomba Serikali mwaka

    moja toka Novemba 2014 ili kulinda mikataba iliyoingiwa kabla

    ya kutunga sheria ya VAT ya mwaka 2014;

  • 20

    Idadi ya watalii waliotembelea mbuga za wanyama kwa kipindi

    2011 hadi 2014 katika nchi za Tanzania, Kenya na Afrika Kusini

    zinaonyesha kwamba Tanzania licha ya kutotoza VAT kwenye

    huduma hii bado imetembelewa na watalii wachache kuliko nchi

    hizo kama ifuatavyo:

    Serikali inapendekeza kutoza VAT kwenye huduma za utalii kwa

    sababu VAT sio kigezo kikubwa kinachoangaliwa na Mtalii wakati

    anafanya maamuzi kufanya utalii. Baadhi ya vigezo muhimu

    vinavyoangaliwa ni vivutio, usalama, huduma kwa watalii na hali

    ya usafiri.

    Hoja Na.9: Serikali ina mkakati gani wa kukabiliana na tatizo la

    watoa huduma kutoza bei kwa kutumia fedha za kigeni kama Dola

    ambalo linapelekea kushuka kwa thamani ya shilingi?

    Ufafanuzi:

    Mheshimiwa Spika,

    Dollarization ni matumizi ya sarafu ya kigeni katika nchi moja

    sambamba na sarafu ya nchi hiyo;

    Mwaka

    Idadi ya Watalii

    Tanzania Hakuna VAT

    Kenya Kuna VAT

    Afrika Kusini Kuna VAT

    2011 867,994 1,750,000 8,339,000

    2012 1,077,058 1,619,000 9,188,000

    2013 1,095,884 1,434,000 9,537,000

    2014 1,140,156 1,261,000 9,549,000

  • 21

    Matumizi makubwa ya fedha za kigeni katika uchumi

    husababishwa na mambo kadhaa yakiwemo vita vya muda mrefu

    katika nchi, kuongezeka kwa mfumuko wa bei na kuporomoka kwa

    thamani ya sarafu ya nchi husika ikilinganishwa na sarafu ya

    kigeni. Kama nilivyoeleza katika hotuba yangu, kushuka kwa

    thamani ya shilingi yetu kulitokana na kuimarika kwa Dola ya

    Kimarekani, kuchelewa kwa upatikanaji wa fedha za kigeni kwa

    ajili ya bajeti ya serikali pamoja na mapato madogo ya fedha za

    kigeni yasiyokidhi mahitaji ya uagizaji wa bidhaa na huduma nje;

    Kwa ujumla, mahitaji ya fedha za kigeni kwa ajili ya uagizaji wa

    bidhaa na huduma nje ya nchi hayawiani na uuzaji wa bidhaa na

    huduma nje. Kwa mfano katika mwaka 2015, thamani ya mauzo

    ya bidhaa na huduma nje ilikuwa Dola za Kimarekani milioni

    9,450.0 ikilinganishwa na Dola milioni 12,528.2 zilizotumika

    kuagiza bidhaa na huduma kutoka nje. Hali hii inasababisha

    kuongezeka kwa nakisi ya urari wa biashara ya bidhaa na

    huduma;

    Mwenendo wa thamani ya Shilingi umekuwa ni chanzo kikuu kwa

    wafanya biashara nchini kupanga bei za bidhaa na huduma zao

    kwa fedha za kigeni. Hivyo basi, namna nzuri na endelevu ya

    kupunguza au kuondoa matumizi ya fedha za kigeni katika

    matangazo ya bei au malipo ya bidhaa na huduma mbalimbali

    kwenye soko la ndani ni kuimarisha thamani ya Shilingi yetu na

    kuendelea kudhibiti mfumuko wa bei. Hali hii itawezekana kwa

    kuendelea kutekeleza sera madhubuti ya fedha na kuhakikisha

  • 22

    kunakuwa na ongezeko la uzalishaji wa chakula pamoja na

    kuboresha usambazaji wa chakula nchini. Hii inajumuisha pia

    kuboresha miundombinu itakayowezesha kilimo cha umwagiliaji na

    kusafirisha chakula kirahisi kutoka sehemu zenye ziada kwenda

    sehemu zenye upungufu;

    Aidha, kuongeza uzalishaji wa bidhaa za mauzo nchi za nje

    kutapunguza nakisi katika urari wa biashara ya bidhaa na huduma

    nchi za nje na hivyo kusaidia kudhibiti kuporomoka kwa thamani

    ya Shilingi. Hivyo basi, kupunguza matumizi ya fedha za kigeni

    (dollarization) ni suala la muda wa kati linalohitaji kuimarisha sera

    madhubuti za uchumi jumla ikiwa ni pamoja na kuendelea kuweka

    mifumo thabiti itakayoleta ongezeko la haraka la uzalishaji wenye

    tija na hivyo kuongeza mauzo ya bidhaa na huduma nje;

    Si nia ya Serikali kurejesha sera ya udhibiti wa umiliki wa fedha za

    kigeni (administrative de-dollarisation) kwani madhara yake ni

    makubwa na baadhi ya nchi zilishajaribu zikashindwa na hivyo

    kurudisha sera ya soko huria. Udhibiti wa umiliki wa fedha za

    kigeni utaleta ushawishi kwa watanzania kutunza fedha za kigeni

    katika mabenki ya nje kinyume na sheria (capital flight). Hii

    itasababisha upungufu mkubwa wa fedha za kigeni na hivyo

    kufanya nchi kushindwa kulipia mahitaji yake kutoka nje. Pia, hali

    hii itasababisha kushamiri kwa soko lisilo rasmi (parallel market) la

    fedha za kigeni cf. IMF (2015) Dollarization in SSA: Experience

    and Lessons;

  • 23

    Serikali itaendelea kusimamia kwa karibu kuhakikisha kwamba

    matumizi ya fedha za kigeni katika uchumi wetu yanafanyika kwa

    kufuata utaratibu uliowekwa kisheria. Sheria ya Benki Kuu ya

    mwaka 2006, sehemu ya tatu, kipengele cha 26, inatamka wazi

    kuwa shilingi ya Tanzania itakubalika na kutumika kama fedha

    halali kwa malipo (legal tender) ndani ya nchi yetu. Hii

    inamaanisha kuwa shilingi ya Tanzania ndiyo fedha pekee ambayo

    haiwezi kukataliwa na mtu yeyote kwa malipo halali ndani ya nchi

    yetu. Hivyo, ni kosa kukataa kupokea shilingi ya Tanzania kwa

    malipo halali nchini; na

    Vile vile, Sheria ya Usimamizi wa Fedha za Kigeni ya mwaka 1992

    (The Foreign Exchange Act, 1992) inaruhusu mtu yeyote kupokea,

    kumiliki na kutumia fedha za kigeni kwa shughuli zake za

    kiuchumi. Vile vile, Sheria hiyo inatamka kwamba mtu yeyote

    anaruhusiwa kuwa na akaunti ya fedha za kigeni katika benki

    iliyoruhusiwa na Benki Kuu kwa ajili hiyo.

    Hoja Na.10: Serikali ipunguze kukopa katika mabenki ya ndani ili

    kutoa fursa kwa sekta binafsi kupata mikopo.

    Ufafanuzi:

    Mheshimiwa Spika,

    Nakisi ya bajeti kwa mwaka 2016/17 ni asilimia 4.5 ya Pato la

    Taifa ikilinganishwa na asimilia 3.7 mwaka 2013/14, asilimia 3.6

    mwaka 2014/15 na asilimia 4.2 mwaka 2015/16. Kiwango cha

    nakisi ya bajeti kimeongezeka kwa asilimia 0.3 ya Pato la Taifa

  • 24

    ikilinganishwa na mwaka 2015/16. Ongezeko hilo limetokana na

    nia nzuri ya Serikali ya kutekeleza kwa dhati Mpango wa pili wa

    maendeleo wa miaka mitano;

    Kigezo kimojawapo cha uchumi mpana katika kuanzishwa kwa

    Umoja wa Fedha wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, ni kuwa na

    kiwango cha nakisi ya bajeti kwa Pato la Taifa cha asilimia 3 pindi

    ifikapo 2021/22. Katika kutekeleza hili, Serikali imepanga

    kupunguza kiwango cha nakisi hatua kwa hatua bila kuathiri

    utekelezaji wa bajeti;

    Katika mwaka 2016/17, Serikali imepanga kuziba nakisi ya bajeti

    ya asilimia 4.5 ya Pato la Taifa kwa kukopa kutoka katika vyanzo

    vya ndani na nje. Kati ya kiasi hicho, asilimia 3.0 ya Pato la Taifa

    itakopwa kutoka vyanzo vya nje na asilimia 1.5 ya Pato la Taifa

    itakopwa kutoka katika vyanzo vya ndani. Ukopaji huo hufanyika

    kwa kuuza hatifungani kwenye soko la ndani la fedha badala ya

    kukopa moja kwa moja kwenye benki za biashara; na

    Kwa maana hiyo, kiasi kitakachokopwa kutoka soko la ndani

    kinazingatia ukomo wa ukopaji ambao hauathiri utoaji wa mikopo

    kwa sekta binafsi ambapo mikopo kwa sekta binafsi imekuwa

    ikiongezeka kwa zaidi ya asilimia 20 kwa mwaka. Ongezeko hili

    linawiana na lengo la ukuaji wa mikopo kwa sekta binafsi kama

    ilivyoainishwa katika Tamko la Sera ya Fedha. Aidha, kiwango cha

    mikopo ambayo imekuwa inayotolewa na benki za biashara kwa

    sekta binafsi ni zaidi ya asilimia 80 ya mikopo yote, wakati mikopo

  • 25

    inayotolewa na benki za biashara kwa Serikali ni chini ya 2%

    Hoja Na. 11: Kuondolewa kwa misamaha ya kodi katika maduka

    na migahawa ya vyombo vya ulinzi na usalama kunaondoa

    motisha katika taasisi hizo. Ikiwa msamaha wa kodi utafutwa,

    bidhaa na vifaa vilivyopo katika bohari za majeshi yetu

    zitapelekwa wapi? Na zipo kiasi gani?

    Ufafanuzi:

    Mheshimiwa Spika,

    Uamuzi wa Serikali wa kuwapa motisha watumishi wa vyombo vya

    ulinzi na usalama bado upo palepale. Mapendekezo ya kuondoa

    msamaha wa kodi katika maduka na migahawa ya vyombo vya

    ulinzi na usalama ni kutokana na misamaha hiyo kutumika vibaya.

    Ili kuondoa kasoro hiyo, Serikali imeamua kuweka utaratibu wa

    kuwalipa posho watumishi wa vyombo vya ulinzi na usalama ili

    wanufaike moja kwa moja kama walengwa. Kiasi cha posho

    atakayolipwa askari kitakokotolewa baada ya mashauriano na

    vyombo husika.

    Serikali inakamilisha utaratibu wa bidhaa ambazo zimesamehewa

    kodi katika maduka yote ya vyombo vya ulinzi na usalama.

    Utaratibu huo utakapokamilika wahusika watajulishwa.

  • 26

    Hoja Na.12: Kodi kwenye “transit goods” ni kinyume na taratibu

    kwa kuwa kodi hiyo hulipwa na mlaji. Hii itasababisha waagizaji

    wa mizigo kuhamia bandari nyingine za Beira na Mombasa.

    Ufafanuzi:

    Mheshimiwa Spika,

    Sheria ya VAT ya Mwaka 2014 imeweka viwango viwili vya kutoza

    kodi ambavyo ni asilimia 18 kwa bidhaa na huduma zinazotumika

    hapa nchini na asilimia 0 pale bidhaa na huduma inaposafirishwa

    nje ya nchi (Exported);

    Huduma zinazotolewa kwenye mizigo inayosafirishwa kwenda nchi

    za jirani kupitia Tanzania siyo “exports” bali zinatolewa na

    kutumiwa ndani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa

    maana kodi ya ongezeko la thamani (VAT) haitozwi kwenye transit

    goods bali hutozwa kwenye huduma ambapo mtumiaji na mtoaji

    wako Tanzania. Huduma hizi zinaweza kutolewa mahali popote

    ndani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na siyo bandarini tu,

    na hivyo ni sahihi kabisa huduma hizi kutozwa asilimia 18;

    Utafiti uliofanywa kubaini kama kutoza kodi ya VAT huduma hizi

    kunaathiri biashara kwenye bandari umeonesha kwamba katika

    kipindi cha Julai, 2015 hadi April, 2016 mizigo iliyopita kwenye

    bandari ya Dar es Salaam imepungua kwa asilimia 15 ukilinganisha

    na mizigo iliyopita katika Mwaka wa Fedha 2014/15 katika kipindi

    kama hicho. Katika Bandari ya Mombasa ambapo huduma hizi

    zimesamehewa kodi ya VAT mizigo imepungua kwa asilimia 25

  • 27

    katika kipindi hicho. Kwa ujumla biashara ulimwenguni kote

    imeshuka katika kipindi hiki, na hivyo kuathiri ukuaji wa uchumi

    jumla; na

    Kwa misingi hiyo si sahihi kusema kwamba kutoza kodi ya VAT

    kwenye huduma zinazotolewa kwenye mizigo inayosafirishwa

    kwenda nchi jirani ndicho chanzo cha kushuka kwa biashara katika

    bandari zetu.

    Hoja Na.13: Serikali iangalie upya mfumo wa “Single Customs

    Territory” unaodaiwa kusababisha kupungua kwa mapato ya

    bandari kutokana na baadhi ya nchi jirani kuepuka kutumia

    bandari ya Dar es Salaam.

    Ufafanuzi:

    Mheshimiwa Spika,

    Mfumo wa “Single Customs Territory (SCT)” ulianza kutumiwa na

    nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki. Mfumo huu

    ulionesha manufaa makubwa katika kuwezesha biashara na

    kudhibiti uvujaji wa mapato baina ya nchi husika. Mfumo huu

    huruhusu wafanyabiashara wanaotumia bandari zetu kupitisha

    mizigo kwenda nchi jirani kulipa kodi kwenye nchi zao kwanza na

    pindi mzigo huo unapowasili bandarini na kujiridhisha kuwa kodi

    husika zimelipwa, mzigo huo huruhusiwa na hivyo kuepusha

    uwezekano wa kuingizwa nchini bila kulipiwa kodi. Utaratibu huu

    pia hurahisisha uondoshaji wa kadhia forodhani. Mfano mzuri wa

    mafanikio ya mfumo huu ni mizigo inayokwenda Rwanda kwani

  • 28

    imeongezeka kwa asilimia 16 kwa kipindi cha kuanzia Julai 2015

    hadi Aprili 2016 ukilinganisha na kipindi kama hicho katika mwaka

    wa fedha 2014/15. Pia muda wakusafirisha mzigo kutoka muda wa

    kuingia na kutoka (from entry to exit) umepungua;

    Mfumo huu wa SCT kwa mizigo inayokwenda Jamhuri ya

    Kidemokrasia ya Congo (DRC) umeanza kutumika kufuatia

    makubaliano kati ya serikali za nchi hizi mbili. Lengo lake ni

    kuharakisha biashara kwa kupunguza muda wa kutoa na

    kusafirisha mizigo kwenda DRC na kudhibiti mapato kwa nchi zote

    mbili. Hivyo kushuka kwa biashara kati ya Tanzania na nchi jirani

    hakujasababishwa na SCT;

    Kwa upande mwingine, dunia imeshuhudia kupungua kwa

    biashara ya kimataifa katika kipindi hiki ambako kumesababishwa

    na kudorora kwa uchumi wa China, kushuka kwa bei ya bidhaa

    (commodities) na mafuta ikiwa pamoja na madini mbalimbali.

    Hivyo, kupungua kwa mizigo inayokwenda nchi jirani na ile

    inayotumika hapa nchini, hakujaiathiri Tanzania peke yake bali

    hata bandari ya Mombasa mizigo ya nchi jirani yaani transit

    ilipungua kwa asilimia 25 kwa kipindi cha kati ya Julai 2015 hadi

    Machi 2016 ikilinganishwa na kipindi kama hicho mwaka 2014/15.

    Utafiti uliofanywa hivi karibuni na TRA/Serikali umebainisha

    sababu za muda mfupi na muda mrefu zilizosababisha kupungua

    kwa mizigo kwenye bandari ya Dar es Salaam ikiwa ni pamoja na

    mizigo inayokwenda nchi jirani na ile kwa ajili ya matumizi ya

    ndani ya nchi (imports);

  • 29

    Sababu za muda mfupi ni pamoja na:- Maandalizi ya Uchaguzi

    Mkuu kwenye Nchi za kanda yetu kama vile Tanzania, Uganda,

    Burundi, machafuko nchini Burundi na Sudan Kusini, kushuka kwa

    bei ya shaba katika soko la dunia kuliathiri uchumi wa Zambia na

    hivyo kushuhudia kupungua kwa mizigo ya kwenda na kutoka

    Zambia, na maboresho ya miundombinu yaliyofanywa na nchi ya

    Msumbiji na Afrika kusini kwa mfano Msumbiji imejenga reli ya

    standard gauge na kuboresha bandari na hivyo kuifanya bandari

    kuwa na miundombinu bora ukilinganisha na bandari yetu. Hali hii

    imeifanya bandari ya Beira kupendelewa zaidi na nchi jirani;

    Sababu za muda mrefu ni pamoja na:- Ufanisi mdogo wa bandari

    ya Dar es Salaam ukilinganisha na bandari zingine, miundombinu

    hafifu ya kusafirisha mizigo hususan kwa njia ya reli na hivyo

    kufanya njia pekee ya uhakika kusafirisha mizigo kuwa ni barabara

    ambayo ni ghali zaidi ukilinganisha na reli; na

    Serikali ya Awamu ya Tano imedhamiria kikamilifu kuondokana na

    changamoto hizo ikiwa ni pamoja na kuboresha huduma za

    bandari na kuimarisha miundombinu ya usafirishaji ikiwa ni

    pamoja na kujenga reli ya kati kwa kiwango cha standard gauge.

  • 30

    Hoja Na.14: Tamko la kufuta retention kwenye Taasisi za

    kimkakati kama TPDC, Serikali ikishindwa kupeleka fedha kwa

    wakati, itapoteza mapato mengi kwa sababu watashindwa

    kusimamia kwa ufanisi mapato kutoka kwa wawekezaji.

    Ufafanuzi:

    Mheshimiwa Spika,

    Utaratibu wa kubakiza sehemu ya mapato (Retention) ulikuwa na

    lengo la kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa shughuli kwa

    baadhi ya Wizara na Taasisi. Katika baadhi ya Wizara na Taasisi

    hizo ufanisi wa ukusanyaji maduhuli umeongezeka;

    Hata hivyo, kumejitokeza dosari katika utekelezaji wa utaratibu

    huo, ikiwa ni pamoja na matumizi makubwa yasiyowiana na

    majukumu ya msingi na kutochangia inavyostahili katika mfuko

    mkuu wa Serikali; na

    Ili kurekebisha dosari na kuhakikisha kuwa Taasisi husika zinapata

    fedha kwa wakati, Serikali imeelekeza Taasisi hizo kuwasilisha

    mpango kazi na mtiririko wa mahitaji ya fedha (action plan and

    cash flow), vigezo ambavyo vitazingatiwa katika utoaji wa fedha

  • 31

    Hoja Na. 15 Ushuru wa Forodha kwenye Sukari ya Viwandani

    Ufafanuzi:

    Mheshimiwa Spika,

    Katika ukurasa wa 71 kwenye kitabu cha Hotuba ya Bajeti

    2016/17 niliyoisoma hapa Bungeni nilieleza kuwa, waagizaji wa

    sukari ya viwandani watatakiwa kulipa ushuru wa asilimia 15

    kwenye sukari wanayoagiza badala ya asilimia 10 wanayolipa sasa

    katika mwaka wa fedha 2015/16. Hilo lililenga kutekeleza

    maamuzi ya Baraza la Mawaziri wenye dhamana ya masuala ya

    fedha wa Jumuiya ya Afrika Mashariki ya kupunguza msamaha

    kwenye sukari ya viwanda hatua kwa hatua hadi kufikia asilimia 25

    kama ifuatavyo: mwaka 2016/17 kiwango kitakuwa asilimia 15,

    2017/18 kiwango kitakuwa cha asilimia 20 na 2018/19 kiwango

    kitakuwa asilimia 25.

    Mheshimiwa Spika, pamoja na kuwa maamuzi ya kuanza kutoza

    ushuru wa forodha wa asilimia 15 kwenye sukari inayoingizwa

    nchini kwa matumizi ya viwanda ulikuwa ni uamuzi wa pamoja wa

    mawaziri wenye dhamana ya masuala ya fedha wa Jumuiya ya

    Afrika Mashariki ni Tanzania pekee ndiyo ingetekeleza

    maamuzi haya katika mwaka wa fedha 2016/17. Nchi za

    Burundi, Kenya na Uganda zimeomba muda wa kujiandaa ili

    waweze kuanza kutekeleza hatua hii katika mwaka wa fedha

    2017/18. Rwanda wanatumia mfumo tofauti ambapo sukari yote

    hutozwa asilimia 25 badala ya kutumia ushuru wa forodha wa

    asilimia 100 au Dola za Marekeni 460 kwa tani moja kwa

  • 32

    kutegemea kiwango kipi ni kikubwa zaidi. Sababu ya nchi hizi

    kutotumia kiwango hicho cha ushuru wa forodha ni ukweli kuwa

    bidhaa hizi hazizalishwi ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki.

    Aidha, ili kujiandaa kwa utekelezaji wa hatua hii, Kenya imepewa

    unafuu wa ushuru wa forodha kwa kuruhusiwa kuingiza sukari

    ghafi kwa kutumia kiwango cha asilimia 0 badala ya asilimia 100

    au Dola za Marekani 460 kwa tani kwa kipindi cha mwaka mmoja.

    Baada ya kupokea maoni ya watengenezaji wa vinywaji pamoja na

    kutafakari juu ya umuhimu wa bidhaa hiyo ambayo hutumika

    kama malighafi ya viwanda vyetu, Serikali imeamua kusitisha

    utekelezaji wa hatua hii hadi mwaka wa fedha 2017/18 kama

    ilivyo kwa nchi nyingine za Jumuiya ya Afrika Mashariki. Hata

    hivyo, Serikali itaendelea kuwataka watumiaji wa sukari hii

    kuendelea kulipia kodi ya asilimia 25 kwanza na kurejeshewa

    asilimia 15 baada ya kuthibitisha uhalali wa matumizi.

    Hoja Na.16: Wizara ya Fedha na Mipango ijihadhari na madalali

    wa mikopo (transaction agents) maana wataongeza gharama za

    mikopo.

    Ufafanuzi:

    Mheshimiwa Spika,

    Ukopaji wa fedha unafanywa kwa mujibu wa Sheria ya Mikopo,

    Dhamana na Misaada Sura 134. Sheria hiyo imetoa Mamlaka kwa

    Waziri wa Fedha na Mipango kukopa mikopo ya ndani na nje kwa

    niaba ya Serikali. Kwa mujibu wa taratibu zilizoainishwa katika

    sheria hiyo, Waziri wa Fedha na Mipango hujadiliana moja kwa

  • 33

    moja na wakopeshaji ambao wanaweza kuwa ni Nchi (Bilateral

    Creditor), Benki moja moja au kundi la mabenki;

    Hata hivyo, kutokana na muundo (structure) wa soko la fedha la

    ndani au la kimataifa, wakati mwingine Waziri wa Fedha anaweza

    akateua taasisi nyingine kumsaidia ili kurahisisha upatikanaji wa

    fedha kutoka soko la fedha husika. Mathalan, kwa sasa Benki Kuu

    ya Tanzania inatumika kama wakala (Agent) wa Serikali katika

    kuuza Hati Fungani na Dhamana za Serikali na kuiwezesha Serikali

    kupata Fedha kutoka Soko la Ndani;

    Kwa upande wa soko la fedha la kimataifa, mikopo mikubwa

    huchangiwa na taasisi nyingi za fedha yakiwemo mabenki na

    wakopeshaji wengine. Taasisi hizo huteua benki au taasisi moja

    miongoni mwao kuwa Wakala yaani Agent/lead arranger au lead

    manager kuwasikilisha mabenki hayo katika majadiliano na

    mkopaji. Huu ni utaratibu wa kawaida kwenye masoko ya fedha

    ya kimataifa na hufanya hivyo ili kurahisisha majadiliano na

    upatikanaji wa fedha kwa wakati;

    Sifa za Wakala huyo anayechaguliwa na mabenki au wawekezaji

    kwenye soko la fedha la kimataifa lazima ni pamoja na kuwa

    uwezo wa kuitangaza nchi kikamilifu katika soko la fedha la

    kimataifa hivyo kuifanya nchiyo kupata fedha na kwa gharama

    nafuu ya soko, kwa upande mwingine, Wakala huyo anatakiwa

    awe na taarifa za kutosha za mkopaji ikiwemo hali ya uchumi,

    siasa na masuala ya kijamii ya nchi husika na uwezo wa nchi hiyo

  • 34

    kurejesha mikopo. Aidha, mkopaji lazima ajiridhishe na kukubali

    kutumia Wakala huyo; na

    Utaratibu huu hutoa uhakika kwa Serikali kupata mikopo kwa

    masharti yanayokubalika baina ya pande mbili zinazo husika. Kwa

    mujibu wa Sheria ya Mikopo, Dhamana na Misaada SURA 134.

    Sheria hii imeweka utaratibu maalum wa kuufuata wakati wa

    kukopa. Kwa mujibu wa Sheria hii kuna Kamati Maalum ambazo

    huchambua masharti ya kila mkopo na kujadiliana na wakopeshaji

    na baada ya majadiliano kukamilika, Kamati hizi ndizo zinamshauri

    Waziri wa Fedha na Mipango kukopa mkopo husika.

    Hoja Na.17: Serikali ishirikishe Kamati ya Kudumu ya Bunge ya

    Bajeti katika maandalizi ya bajeti.

    Ufafanuzi:

    Mheshimiwa Spika,

    Serikali imekuwa ikiishirikisha Kamati ya Bunge ya Bajeti na

    Waheshimiwa Wabunge katika hatua mbalimbali za maandalizi ya

    bajeti. Ushirikishwaji huo hufanyika katika hatua zifuatazo:

    Maandalizi ya Mwongozo wa Mpango na Bajeti Kamati za Kudumu

    za Bunge za Kisekta; na

    Kamati ya Bunge ya Bajeti, ambayo hushirikishwa kikamilifu katika

    kuchambua makadirio ya bajeti ya Serikali; kupitia rasimu ya

    mfumo wa bajeti; kupitia hoja za kibajeti zinazoibuka kwenye

  • 35

    sekta mbalimbali; kushauriana na Serikali kuhusu vyanzo vipya vya

    mapato.

    Hata hivyo, ili kulinda kazi ya Bunge ya kuishauri na kuisimamia

    Serikali ni muhimu kwamba Bunge lisijiingize katika kazi za

    kiutendaji katika maandalizi ya bajeti na badala yake Bunge

    lichambue na kushauri kuhusu mapendekezo ambayo tayari

    yanakuwa yameridhiwa na Serikali.

    F: HITIMISHO

    8. Mheshimiwa Spika, tuna dhamana ya kuleta mabadiliko makubwa

    katika uendeshaji wa shughuli zote za umma na matumizi ya rasilimali za

    Taifa ili kuwezesha kupiga hatua kubwa ya kuiondoa nchi yetu katika

    umaskini. Katika hili, kila mwananchi atambue wajibu wake wa kufanya

    kazi kwa bidii, kuwa na nidhamu ya hali ya juu katika nyanja zote na

    uzalendo kwa Taifa letu.

    9. Mheshimiwa Spika, nirudie tena kuzielekeza Wizara, Idara

    zinazojitegemea, Taasisi na Wakala za Serikali, Sekretarieti za Mikoa na

    Mamlaka za Serikali za Mitaa kuzingatia hatua za kuimarisha ukusanyaji

    wa mapato; usimamizi wa matumizi ya Serikali na hatua za kupunguza

    gharama; na kulipa na kuzuia ongezeko la madeni ya Serikali. Serikali ina

    dhamira ya dhati kabisa ya kuchukua hatua hizo na ninaomba Watanzania

    wote watambue kwamba ni lazima kujinyima, kujituma na kuvuja jasho ili

    kupata maendeleo na kupunguza utegemezi. Wajibu wa kwanza wa

    kuiendeleza Tanzania ni wa Watanzania wenyewe. Tuna akili za kutosha,

  • 36

    rasilimali nyingi na fursa tele kuifanya Tanzania kuwa nchi ya viwanda na

    Uchumi wa Kipato cha Kati ifikapo 2025.

    10. Mheshimiwa Spika, ninawaomba tena Waheshimiwa Wabunge kuunga mkono hatua zinazoongozwa na Serikali ya Awamu ya Tano

    kuhakikisha kuwa tunaimarisha ukusanyaji wa mapato ya ndani ya kodi na

    yasiyo ya kodi na kuelekeza matumizi kwenye maeneo yenye tija kwa

    manufaa ya watanzania wote.

    11. Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja.