hotuba ya mhe. jakaya mrisho kikwete, rais wa … · 2014. 11. 12. · kati ya mwaka 2002 hadi 2006...

17
HOTUBA YA MHE. JAKAYA MRISHO KIKWETE, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA KWENYE KILELE CHA MAADHIMISHO YA SIKU YA MWALIMU DUNIANI TAREHE 11 OKTOBA, 2006 Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Mh. Margaret Sitta (Mb); Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Mheshimiwa Henry Shekifu (Mb); Makamu wa Rais wa CWT, Ndugu Yahya Msulwa; Waheshimiwa Viongozi wa chama na Serikali; Viongozi wa Vyama vya Wafanyakazi; Wajumbe wa Baraza la Taifa la Chama cha Walimu Tanzania; Walimu wote, Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana: Nianze kwa kutoa shukrani zangu za dhati kwa heshima mliyonipa ya kunialika kushiriki nanyi katika sherehe hizi za maadhimisho ya Siku ya Mwalimu Duniani. Nawashukuru kwa mapokezi mazuri mliyonipa na burudani murua za kwaya na muziki wa Boka Boma Music Band. Nawapongeza wale wote walioshiriki kuandaa maadhimisho haya yaliyofana. Nimefurahishwa sana na niliyoyaona kwenye mabanda ya maonyesho. Pongezi za pekee kwa Chama cha Walimu Tanzania kwa kuendelea kuwaunganisha walimu nchini, na ninawapongeza walimu wote kwa kuadhimisha siku yenu leo hii. Nawaahidi ushirikiano wangu na ule wa wenzangu wote Serikalini.

Upload: others

Post on 24-Jan-2021

1 views

Category:

Documents


0 download

TRANSCRIPT

  • HOTUBA YA MHE. JAKAYA MRISHO KIKWETE, RAIS WA JAMHURI YA

    MUUNGANO WA TANZANIA KWENYE KILELE CHA

    MAADHIMISHO YA SIKU YA MWALIMU DUNIANI TAREHE 11 OKTOBA, 2006

    Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Mh. Margaret Sitta (Mb);

    Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Mheshimiwa Henry Shekifu (Mb);

    Makamu wa Rais wa CWT, Ndugu Yahya Msulwa;

    Waheshimiwa Viongozi wa chama na Serikali;

    Viongozi wa Vyama vya Wafanyakazi;

    Wajumbe wa Baraza la Taifa la Chama cha Walimu Tanzania;

    Walimu wote, Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana:

    Nianze kwa kutoa shukrani zangu za dhati kwa heshima mliyonipa ya kunialika

    kushiriki nanyi katika sherehe hizi za maadhimisho ya Siku ya Mwalimu Duniani.

    Nawashukuru kwa mapokezi mazuri mliyonipa na burudani murua za kwaya na

    muziki wa Boka Boma Music Band.

    Nawapongeza wale wote walioshiriki kuandaa maadhimisho haya yaliyofana.

    Nimefurahishwa sana na niliyoyaona kwenye mabanda ya maonyesho. Pongezi za

    pekee kwa Chama cha Walimu Tanzania kwa kuendelea kuwaunganisha walimu

    nchini, na ninawapongeza walimu wote kwa kuadhimisha siku yenu leo

    hii. Nawaahidi ushirikiano wangu na ule wa wenzangu wote Serikalini.

  • Ndugu viongozi, ndugu wananchi;

    Leo tunawapongeza walimu kwa kuadhimisha siku yao duniani. Hii ni siku

    muhimu kwa walimu. Ni siku ambayo walimu duniani kote hutafakari mahali walipo

    na kule waendako katika kutimiza wajibu wao wa kutoa elimu. Na sisi wadau wengine

    ni fursa ya kuonyesha shukrani na pongezi zetu, kama Taifa, kwa walimu wote nchini

    kwa kazi kubwa wanayoifanya katika kulijenga na kuliendeleza Taifa letu.

    Nchi yetu ni kubwa na maeneo mengi yanapishana kwa viwango vya

    maendeleo, lakini Mwalimu yuko katika kila kona ya nchi hii. Walimu ndio huwafunda

    na kuwalea raia na viongozi wa kesho wa taifa letu.

    Vilevile, walimu ndio wanaotutengenezea viongozi katika fani mbalimbali za

    taaluma na ujuzi. Walimu ndio wanaotujengea nguvu kazi ya kutumainiwa ya Taifa

    letu. Walimu ndio wanaoijenga haiba ya taifa. Nakubaliana nanyi kabisa kwamba

    walimu ndio chimbuko la taifa na utaifa. Miongoni mwa walimu ndio

    wametoka viongozi wengi wa nchi yetu wakiwemo Wabunge na Mawaziri. Hata Rais

    wetu wa kwanza Baba wa Taifa, hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Rais

    wetu wa pili Mzee Ali Hassan Mwinyi walikuwa walimu.

    Ni ukweli uliodhahiri kwamba, aina ya walimu tunaokuwa nao, inaamua aina

    ya Taifa tunalolijenga. Kwahiyo basi, kwa Serikali na jamii yote kwa jumla, kutambua

    na kuheshimu nafasi ya Mwalimu katika ujenzi na maendeleo ya Taifa letu, ni jambo

    muhimu sana.

    Ahadi yangu kwenu ni kwamba tutaendelea kuutambua, kuuheshimu na

    kuuenzi mchango wa walimu kwa Taifa letu. Tunatambua kuwa wengi wenu

    mnafanya kazi katika mazingira magumu. Serikali haitachoka kuzifanyia kazi kero za

    walimu na kutafuta njia mbalimbali za kuwasaidia.

  • Ndugu Makamu wa Rais wa CWT, Ndugu Walimu;

    Mimi na wenzangu Serikalini tunalipa kipaumbele cha juu suala zima la Elimu

    nchini. Mipango na malengo yetu katika Sekta ya Elimu inaongozwa na Malengo ya

    Milenia ya Elimu, Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2025, Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya

    Mwaka 2005 na Mpango wa Kukuza Uchumi na Kuondoa Umaskini Tanzania

    (MKUKUTA). Nia yetu ni nini basi?

    Moja, ni kuhakikisha upatikanaji wa elimu kwa wote.

    Mbili, ni kuhakikisha kuwa kunakuwa na usawa na haki katika utoaji

    elimu;

    Tatu, kuona kuwa ubora wa elimu inayotolewa unaongezwa na

    kuimarishwa;

    Nne, kuhakikisha kuwa rasilimali tunazotenga kwa ajili ya utoaji elimu

    zinatumika kwa ufanisi na kutimiza malengo tunayoyakusudia.

    Tano, tunaimarisha asasi za uongozi na uendeshaji wa Sekta ya elimu;

    Sita, tunaongeza ushirikishwaji wa Wadau mbalimbali wa elimu,

    ikiwemo sekta binafsi katika upangaji sera na mipango ya elimu;

    Ndugu zangu, kwa bahati nzuri, haya vilevile ndiyo malengo ya mipango

    mikubwa ya elimu inayotekelezwa hivi sasa, yaani Mpango wa Maendeleo ya Elimu ya

    Msingi (MMEM) 2002 – 2006 na Mpango wa Maendeleo ya Elimu ya Sekondari (MMES)

    2004 – 2009. Serikali inafanya kila juhudi ili kuhakikisha kuwa mipango hii

    inafanikiwa. Lakini bila ushirikiano wa walimu hatuwezi kufika popote. Nichukue

  • fursa hii kuomba ushirikiano wa walimu wote nchini katika utekelezaji wa MMEM na

    MMES.

    Kuendeleza Ubora wa Elimu

    Ndugu Makamu wa Rais wa CWT;

    Malengo ya Milenia ya Elimu kwa watoto wote wenye umri wa kwenda shule

    ifikapo mwaka 2015 yanasisitiza juu ya ubora wa Elimu itolewayo kwa watoto wote.

    Mwalimu ndiyo raslimali muhimu katika kuyafikia malengo yetu tuliyojiwekea katika

    Sekta ya Elimu likiwemo lile la ubora wa elimu. Hivyo basi, kauli mbiu yenu ya “Kila

    Mwanafunzi Anahitaji Mwalimu Bora” ni sahihi. Ni kauli muafaka kwa kipindi hiki

    tulicho nacho.

    Ndugu zangu;

    Kama nilivyosema hapo mwanzo, Serikali inamtambua Mwalimu na kuthamini

    sana nafasi yake katika kuchangia maendeleo ya elimu na ya nchi kwa ujumla. Kwa

    ajili hiyo, Serikali itaendelea kuhakikisha kuwa walimu wanaandaliwa vizuri,

    wanaendelezwa kazini, wanaandaliwa mazingira mazuri ya kufanyia kazi na kujali

    maslahi yao.

    RISALA

    Ndugu Makamu wa Rais wa CWT;

    Ninawashukuru sana kwa risala yenu nzuri na iliyowasilishwa vizuri. Nafurahi

    kwamba risala imebainisha vyema mafanikio na matatizo yanayowakabili walimu na

  • kutoa mapendekezo muafaka juu ya hatua za kuchukua. Vilevile mmetaja maeneo

    yanayohitaji mazungumzo na maelewano na Serikali na wadau wengine ili tuweze

    kuyafikia malengo ya kielimu tuliyojiwekea. Napenda kuwahakikishia kuwa

    tumesikia, tumeelewa na tuko tayari kufanya kila tuwezalo kufanya yale yanayoihusu

    Serikali.

    Uboreshaji wa Mishahara ya Walimu

    Ndugu Makamu wa Rais wa CWT;

    Natambua haja na umuhimu wa kuboresha maslahi ya walimu, hasa mishahara

    yao. Tumeanza kuchukua hatua. Katika mwaka huu wa fedha, tumeongeza mishahara

    ya walimu, kama ilivyokuwa kwa kada mbalimbali za utumishi wa

    umma. Tutaendelea kuboresha mishahara ya watumishi wa umma pamoja na walimu

    kadri uchumi wetu unavyokua na hali inavyoruhusu.

    Kwa kuzingatia hilo, tarehe 18 Mei, 2006 Serikali iliunda Tume ya Kuboresha

    Mishahara ya Watumishi wa Umma pamoja na walimu. Tume ilianza kazi rasmi tarehe

    01 Julai, 2006 na kazi yake kubwa ni kufanya uchunguzi kuhusu hali ya Mishahara ya

    Watumishi wa Umma ilivyo sasa na kutoa mapendekezo ya namna ya kuiboresha

    zaidi. Tume hiyo imeshakutana na wadau mbalimbali wakiwemo wawakilishi wa

    walimu wa Shule za Msingi, Sekondari, na vyuo vya Ualimu.

    Kwa upande wa Walimu, tume hiyo inapitia maeneo yafuatayo kwa lengo la

    kushauri namna ya kuboresha mishahara ya walimu:

    Misingi gani itumike kupanga mishahara ya walimu;

    Serikali ifanye nini kuboresha mishahara ya walimu;

  • Mwalimu wa Shule ya Msingi, Sekondari na Chuo ana majukumu gani

    anayoyafanya kuanzia asubuhi hadi jioni;

    Kazi ya mwalimu inaweza kulinganishwa na ipi nyingine katika

    Utumishi wa Umma na kwa nini;

    Mambo gani mengine yazingatiwe katika kuboresha mshahara wa

    mwalimu.

    Tume hii tayari imeanza kupokea maoni na ushauri kuhusu uboreshaji

    wa mishahara ya walimu. Ni matarajio yangu kuwa muda iliyopewa utatosha kabisha

    kuwasilisha mapendekezo muafaka Serikalini. Naomba tuwe na subira Tume imalize

    kazi yake. Nawaahidi kuwa Serikali itaifanyia kazi ipasavyo taarifa ya Tume hiyo.

    Ucheleweshaji wa Mishahara ya Walimu

    Mmelielezea kwa uchungu tatizo la ucheleshwaji mishahara ya walimu.

    Naelewa machungu yenu, na nawaunga mkono. Tatizo hili sasa lina kila dalili ya kuwa

    sugu na kuota mizizi lisipokomeshwa. Bila ya shaka mnakumbuka kwamba Serikali

    ilikwishatoa maelekezo kuwa ifikapo tarehe 25 kila mwezi mishahara ya walimu iwe

    imelipwa. Hata hivyo, bado maelekezo haya hayajatekelezwa kwa ukamilifu. Sababu

    mbalimbali zimekuwa zikitolewa lakini bado hazikidhi haja. Sielewi kwa nini watu

    wanajaribu kuhalalisha kutotimiza ipasavyo wajibu wao kwa jambo linalowezekana.

    Wakati mwingine maelezo yanayohalalisha kutojali na uzembe kwa upande wa

    wenzetu tuliowapa dhamana ya kushughulikia mishahara ya walimu. Bado mimi

    naamini tukijipanga vizuri na kutimiza ipasavyo wajibu wetu tunaweza kulipa

    mishahara ya walimu ifikapo tarehe 25 ya kila mwezi. Ingekuwa vyema basi Wizara ya

    Elimu na Mafunzo ya Ufundi, TAMISEMI, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na

  • HAZINA wakakaa pamoja na kuzungumzia vikwazo na kutafuta njia bora zaidi ya

    kulipa mishahara ya walimu kwa wakati. Katika mazungumzo hayo, wazingatie suala

    la walimu wapya na kuchelewa sana kulipwa mishahara yao.

    Ningependa kupata taarifa kuwa baada ya kikao hicho kero hii itakuwa

    imepatiwa ufumbuzi wa kudumu. Usumbufu wanaopata walimu kufuatilia stahili yao

    unapunguza ari na tija yao kazini. Pia hupunguza mapenzi kwa kazi yao. Ualimu ni

    kazi ya heshima. Tusimfikishe mahali Mwalimu anakopa kila mwezi ili aishi

    wakati akingojea mshahara wake.

    Upandishaji wa Madaraja kwa Walimu

    Ndugu zangu,

    Nimesikia pia kuhusu tatizo la ucheleweshaji wa upandishwaji wa madaraja

    kwa walimu, ambalo nalo linachukua sura ya kuwa sugu. Pia lipo tatizo la

    ucheleweshaji wa marekebisho ya mishahara baada ya kupandishwa madaraja. Wakati

    mwingine mtu anapandishwa madaraja mawili au hata zaidi wakati ambapo hata kwa

    daraja la nyuma alilopandishwa mshahara haujarekebishwa. Kupandishwa daraja

    wakati ukifika na kurekebishiwa na kurekebishiwa mshahara kwa wakati ule ni haki ya

    mtumishi. Kutofanya hivyo ni uonevu. Ni matatizo ambayo napata ugumu

    kuelewa. Isitoshe hakuna maelezo ya msingi kwa nini jatatizo haya yasiishe. Naomba

    sasa iwe ilani ya mwisho. Safari ijayo tupate taarifa ya mabadiliko. Hatuwezi

    kuzungumza jambo hilo hilo kila mwaka.

    Naomba kuitumia nafasi hii kuwakumbusha wahusika kuzingatia muongozo wa

    Serikali wa mwaka 2005 kuhusu kushughulikia malalamiko ya watumishi wa umma

    kuhusu kupandishwa vyeo na kuyashughulikia mapema iwezekanavyo.

  • Ni vyema mamlaka zinazohusika na upandishaji wa vyeo vya walimu zikiwemo Tume

    ya Utumishi wa Umma - Idara ya Huduma ya Walimu, Wizara ya Elimu na Mafunzo

    ya Ufundi na halmashauri za Wilaya na Miji kuhakikisha kuwa zoezi la walimu wote

    wenye sifa kupandishwa vyeo stahili linakamilika kabla ya tathmini ya utendaji wa

    kazi kwa njia ya uwazi (OPRAS) kuanza.

    Madeni ya Walimu

    Ndugu Makamu wa Rais wa CWT;

    Ndugu Walimu;

    Mmelielezea pia tatizo la malimbikizo ya madeni ya walimu. Tunatambua kuwa

    hili ni tatizo la siku nyingi na kuna walimu wengi ambao hawajalipwa kwa muda

    mrefu stahili zao mbalimbali hasa fedha za uhamisho, matibabu, mapunjo ya

    mishahara, gharama za masomo na posho za kikazi na likizo.

    Ndugu zangu Walimu, mkakati wa kulipa madeni ya walimu tunao na

    mchakato wa kufanikisha azma hiyo unaendelea. Mpaka sasa madeni ya walimu wa

    shule za msingi yaliyowasilishwa ni kiasi cha shilingi Bilioni 9.9. Hatua za uhakiki wa

    madeni hayo zinakamilishwa.

    Nawasihi wale wanaofanya kazi hii waongeze kasi ili waimalize mapema

    iwezekanavyo na malipo yafanyike ndani ya kipindi hiki cha mwaka wa fedha 2006/07.

    Fedha yake ipo, kinachosubiriwa ni kupatikana kwa taarifa hizo za uhakiki.

    Kwa upande wa walimu wa Sekondari na Vyuo chini ya Wizara ya Elimu na

    Mafunzo ya Ufundi, madeni yenye thamani ya Shilingi Bilioni 1.1 yaliwasilishwa

    Serikalini. Baada ya uhakiki, madeni ya zaidi ya shilingi milioni 855 yameonekana

  • hayana matatizo (queries) na yatalipwa wakati wowote kuanzia sasa. HAZINA

    imekwishatenga fedha hizo na nimeambiwa wako katika maandalizi ya mwisho ya

    kulipa.

    Nyumba za Walimu

    Ndugu Walimu,

    Nalitambua vyema tatizo kubwa la upungufu wa nyumba za walimu nchini,

    hasa vijijini. Kama mlivyosema katika risala yenu, nyumba zilizopo zinakidhi asilimia

    19.4 tu ya mahitaji. Nakubaliana nanyi kwamba tatizo hili ni mateso makubwa kwa

    walimu. Lakini, napenda kuwahakikishia kuwa hili ni jambo linalonisononesha na mie

    pia. Serikali inalitambua na imeendelea kulichukulia hatua za kukabiliana

    nalo. Mikakati ya muda mfupi wa kati na mrefu ili kupunguza makali yake imewekwa

    na inaendelea kutekelezwa.

    Katika utekelezaji wa MMEM, kwa mfano, jumla ya nyumba 12,590 zimejengwa

    kati ya mwaka 2002 hadi 2006 katika shule za msingi. Aidha, kwa mwaka wa fedha

    2006/07 nyumba 2,000 zinatarajiwa kujengwa katika shule za msingi. Kwa upande wa

    shule za sekondari, jumla ya nyumba 908 zimejengwa katika mwaka wa kwanza wa

    utekelezaji wa Mpango wa MMES, unaoisha mwaka 2009. Kwa mwaka wa fedha

    2006/07 jumla ya nyumba 1,000 zinatarajiwa kujengwa na fedha za ukamilishaji wa

    majengo hayo tayari zimetumwa mashuleni. Aidha, kama mjuavyo, katika Mpango wa

    MMES, kwa nia hiyo hiyo ya kupunguza tatizo hilo, kila yanapojengwa madarasa

    mawili hujengwa nyumba moja ya mwalimu.

  • Mimi na wenzangu Serikalini tunatambua umuhimu wa kuongeza kasi ya ujenzi

    wa nyumba za walimu. Tumedhamiria kufanya hivyo ila kasi yetu inapunguzwa na

    uwezo wetu ukilinganisha na mahitaji mengi ya nchi pamoja na hili la nyumba za

    walimu. Tunawahakikishia kuwa tutaendelea kuwekeza kwenye ujenzi wa nyumba za

    walimu. Serikali pia itaendelea kuwashirikisha wadau mbalimbali wakiwemo wahisani

    wa nje, , mashirika ya Serikali na yasiyo ya Kiserikali na watu binafsi katika ujenzi wa

    nyumba za walimu. Kwa ajili hiyo, kwa mfano, Shirika la Maendeleo ya Jamii (TASAF)

    limejenga nyumba za walimu 264 kati ya mwaka 2001 na 2005. Najua wanaendelea

    kufanya hivyo.

    Tumeanza mazungumzo na wahisani wetu wakubwa juu ya haja ya kuwa na

    mpango maalumu wa kujenga nyumba za walimu nchini. Wazo hilo linapokelewa

    vizuri ila bado tunasubiri uamuzi wa kiutekelezaji. Kwa nafasi hii, nawashukuru

    wadau wote wanaochangia kwa hali na mali katika kupunguza tatizo la nyumba za

    walimu.

    Ubora wa Elimu na Muda wa Mafunzo ya Walimu

    Ndugu Walimu,

    Nimefurahi sana kuona kwamba suala la utoaji wa elimu bora shuleni na

    uhusiano wake na muda wa mafunzo ya walimu na mafunzo kazini mnalitambua na

    kulipa nafasi yake stahiki. Ni jambo muhimu kwamba sote tunashiriki kuchuna bongo

    zetu na kuchangia katika jitihada za kutafuta njia ya kuboresha elimu tunayoitoa kwa

    watoto wetu. Kwa ufahamu wangu, Elimu Bora ni matokeo ya majumuisho ya mambo

    mengi, mwalimu akiwa muhimili mkuu wa ubora huo.

  • Kimsingi ufanisi kwa upande wa Elimu Bora unamtegemea mwalimu

    anayemudu maudhui ya somo, mahiri katika matumizi ya njia za kufundisha na

    kujifunzia masomo yaliyoko kwenye mtaala. Kadhalika, hutegemea mwalimu mwenye

    utambuzi wa mahitaji ya walengwa, mazingira bora ya kujifunzia na walimu kuwa

    mfano wa kuigwa.

    Aidha, natambua pia kwamba mazingira bora ya kufanyia kazi kwa walimu

    yana nafasi ya aina yake katika uwezeshaji wa mwalimu kutumia taaluma yake na

    vipaji vyake alivyojaliwa na Mwenyezi Mungu.

    Uzoefu ndani na nje ya nchi na utafiti wa kielimu unaonesha wazi kuwa Ubora

    wa Mwalimu hutegemea sana mafunzo endelevu baada ya kupata Mafunzo ya Awali

    (tarajali). Tunaweza kuwaweka walimu miaka 2, 3 au hata zaidi katika mafunzo ya

    ualimu, lakini kama hakuna mafunzo ya kufuatilia ni vigumu kupata aina ya walimu

    tunaowataka. Hivyo hatuna budi kuweka mkazo stahiki kwa mafunzo kazini kwa

    walimu wetu.

    Ndugu Walimu, naomba tutambue pia kuwa unapokuwa na mipango ya kuleta

    mabadiliko makubwa katika elimu, aghalabu huna budi kutumia njia mbadala na

    wakati mwingine za dharura kupata mahitaji ya msingi au kutatua matatizo muhimu.

    Mpango wa muda mfupi wa kuandaa walimu ni mfano mmojawapo. Huu ndiyo

    ulikuwa msingi wa kuendesha Mafunzo ya Ualimu Ngazi ya Cheti katika sehemu mbili

    (yaani Chuoni na Shuleni) wakati wote wa utekelezaji wa MMEM. Baada ya mahitaji ya

    haraka ya walimu kupungua, hivi sasa Serikali imerudi tena kwenye kutoa mafunzo ya

    Ualimu kwa miaka miwili.

    Kwa kutumia njia hii mbadala kwa mwaka mmoja tumeweza kuboresha uwiano

    wa mwalimu kwa mwanafunzi kutoka 1:56 (2004) hadi kufikia 1:52 (2006) kitaifa

  • pamoja na kwamba bado zipo tofauti baina ya mikoa na wilaya. Kinachotakiwa sasa ni

    kuendeleza mafanikio yaliyopatikana. Kazi iliyo mbele yetu ni kuimarisha mafunzo

    kwa walimu wetu hawa ili kunoa ubora wao.

    Kazi hiyo tunaendelea nayo. Tumekwishatumia shilingi milioni 880.5

    kugharamia walimu wa Sekondari 655 na wakufunzi 370 kujiendeleza kwenye Vyuo

    Vikuu.

    Pia, nimejulishwa kuwa walimu 21,519 wa Daraja B na C wameendelezwa

    kitaaluma na walipimwa Mei, 2006. Vilevile, Walimu 26,017 wanaendelea na mafunzo

    na watafanya mitihani yao ifikapo Mei, 2007. Nimeambiwa pia kuwa Walimu 42,000 wa

    daraja A wamehudhuria Mafunzo ya Ualimu kazini katika matumizi ya njia shirikishi.

    Kwa hiyo, tunaendelea kufanya juhudi. Nia yetu ni kuhakikisha kwamba Kila

    Mwanafunzi anapata Mwalimu aliye Bora, aliyeandaliwa vyema, kama ambavyo kauli

    mbiu yenu inavyosema.

    Kutokana na umuhimu wa kuendeleza walimu kitaaluma na kitaalamu natoa

    wito kwa mamlaka zote zinazohusika na masuala ya walimu kuhakikisha kuwa fedha

    zote zinazotengwa kwa ajili ya mafunzo zinatumika kama ilivyokusudiwa.

    Waratibu wa Elimu ya Sekondari

    Ndugu Makamu wa Rais wa CWT;

    Elimu ya Sekondari ni muhimu katika maendeleo ya Elimu nchini na katika

    kuleta maendeleo ya kijamii na kiuchumi. Tunashukuru kwamba Elimu ya Sekondari

    inapanuka kwa kasi kubwa nchini. Hii inatupa changamoto ya kuendelea na jitihada za

  • kuiboresha. Hivyo, katika kuiboresha Elimu hiyo, tumeamua kusogeza huduma karibu

    na walimu. Utaratibu wa kuwa na Waratibu wa Elimu ya Sekondari katika ngazi ya

    wilaya ni hatua ya awali ya kufikia azma hiyo.

    Vifaa vya Kufundishia na Kujifunzia

    Ndugu zangu, Walimu,

    Napenda sasa kuzungumzia suala la upatikanaji wa vifaa vya kufundishia na

    kujifunzia. Elimu bora na Mwalimu Bora huchangiwa sana na upatikanaji wa nyenzo

    na vifaa vya kufundishia. Vilevile, kuwa na mwanafunzi bora kunategemea upatikanaji

    wa vifaa vya kujifunzia pamoja na walimu bora na mazingira mazuri ya shuleni na

    nyumbani.

    Tunatambua ukubwa wa matatizo ya upatikanaji wa vifaa vya kufundishia na

    kujifunzia hasa katika kipindi hiki ambapo shule zinaongezeka na ubora wa elimu ni

    agenda yetu muhimu. Tunaendelea na juhudi za kulikabili tatizo hili. Tumenunua

    vitabu vya kiada vya kutosha sasa na kupunguza uwiano wa mwanafunzi kwa kitabu

    kwa shule za msingi kutoka 1:20 mwaka 2000 hadi 1:3 mwaka huu.

    Tutaendelea kutoa Ruzuku ya Uendeshaji kwa shule za msingi kwa ajili ya

    ununuzi wa vifaa vya kufundishia na kujifunzia. Katika mwaka huu wa fedha,

    tumetenga jumla ya shilingi bilioni 44.8 kwa ajili ya vifaa vya kufundishia na

    kujifunzia. Hata shule za Sekondari zisizokuwa za Serikali nazo tumeamua

    kuzichangia. Tumetenga shilingi milioni 250 kwa ajili hiyo. Serikali itaendelea

    kuboresha mazingira ya kufundishia na kujifunzia katika ngazi zote ili kufikia lengo la

    kutoa elimu bora kwa watoto wetu.

  • TATIZO LA UKIMWI

    Ndugu Makamu wa Rais wa CWT,

    Ndugu Walimu,

    Nimefarijika sana kuona kuwa, katika risala yenu, mmeongelea suala la

    UKIMWI. UKIMWI bado ni tishio la maisha ya Watanzania wote ikiwa ni pamoja na

    walimu. Ugonjwa huu unatishia kuhatarisha na kudhoofisha juhudi tunazozifanya za

    kupunguza pengo la upungufu wa walimu. Kila mwaka, UKIMWI unatupokonya

    walimu wengi. Hatuna budi kuongeza juhudi za kupambana na maradhi haya hatari.

    Nawaomba walimu muamue kukataa kuambukizwa UKIMWI.

    Ugonjwa huu unaepukika, na nitashangaa sana kama yupo mwalimu asiyejua

    njia za kuepuka UKIMWI. Ukweli ni kwamba jamii inawategemea walimu kuwaandaa

    watoto wao wajiepushe na UKIMWI. Siamini kuwa wapo walimu wasiojua A,B,C za

    kujikinga na UKIMWI: Abstain, Be faithful or Use condom. Sio mambo mapya.

    Wasiokuwa na ndoa, wasubiri; wenye ndoa, wawe waaminifu – hata wenye wapenzi

    hivyo hivyo. Na wale watakaoshindwa kabisa wahakikishe wanapofanya tendo la ndoa

    wanafanya hivyo kwa usalama na usalama huo unafahamika. Nawasihi tuzingatie haya

    kwani tatizo hili ni kubwa na linalotishia maangamizi.

    Ndugu Makamu wa Rais wa CWT,

    Serikali inao Mpango wa Elimu ya UKIMWI katika Shule za Msingi, Sekondari,

    Vyuo na sehemu za kazi. Kupitia mpango huu, walimu hupata uelewa wa mambo

    mbalimbali kuhusu UKIMWI ikiwa ni pamoja na elimu ya matumizi ya dawa za

  • kurefusha maisha. Ninaelewa kuwa si walimu wote wanaopata mafunzo hayo

    vyuoni. Hata hivyo, tunawategemea hao wachache kuwaelimisha wengine

    wanaporudi vituoni mwao ili nao wajumuike katika mapambano haya ya kufa na

    kupona.

    Kwa kuwa Chama cha Walimu kinawakilisha walimu walio wengi, ninashauri

    Wizara ya Elimu na Mafunzo ya ufundi wakae pamoja na CWT kuona ni jinsi gani

    wanaweza kushirikiana kukabiliana na janga hili.

    Pengine niitumie nafasi hii kuwaarifu kuwa mke wangu, ambaye ni Mwalimu

    mwenzenu, ameamua kutumia muda wake wa kuwa likizo bila malipo kujishughulisha

    na juhudi za kupunguza maambukizi mapya ya UKIMWI kwa vijana. Nafahamu pia

    kwamba anayo nia ya kutumia sehemu ya muda wake kuchangia katika mapambano

    dhidi ya maradhi haya miongoni mwa walimu wenzake. Mimi na yeye tunatambua

    kuwepo kwa wanaharakati wa mapambano haya miongoni mwenu. Ameamua

    kushirikiana nanyi, kufanya kazi nanyi. Nawaomba mumpokee, mshirikiane naye.

    Nadhani anaweza kuwa wa msaada kwa kiasi fulani.

    Ndugu zangu,

    Katika risala yenu mmeongelea pia masuala mengine ya maslahi na haki zenu

    kama walimu. Yale yote yahusuyo matatizo ya Mfuko wa Bima ya Afya, Malipo ya

    Pensheni, kuundwa kwa chombo cha majadiliano kati ya CWT na Serikali, nimeyasikia,

    Waziri wa Elimu ameyasikia na viongozi wa Chama cha Walimu nao wameyasikia.

    Bahati nzuri sana mnaye Waziri anayejua kwa undani kero na matakwa ya

    Walimu. Yeye ni Mwalimu mwenzenu na kwa miaka kadhaa amekuwa mwanaharakati

    mwenzenu wa kupigania haki za wafanyakazi (sijui baada ya kuwa Waziri wa Elimu

    kama bado ni mwanaharakati).

  • Mnacho Chama imara cha Walimu Tanzania, na, nawahakikishia kuwa mnayo

    Serikali inayosikia, inayosikiliza, inayojali na iliyo tayari kuchukua hatua. Tunayo

    dhamira ya dhati ya kuboresha elimu kwa kuongeza walimu, kuboresha hali ya shule,

    maslahi ya walimu, pamoja na mazingira yao ya kufanyia kazi. Tuendelee kuzungumza

    na kushauriana.

    Nimefurahi kwamba mmesema kwenye risala yenu pia kuhusu utekelezaji wa

    kuundwa kwa chombo cha majadiliano kati ya Serikali na Chama cha Walimu

    Tanzania. Ni kweli Tanzania imeridhia mkataba wa Shirika la Kazi Duniani ILO No. 98

    unaohusu haki za wafanyakazi kujadiliana na waajiri kuhusu maslahi na mazingira

    bora ya kazi. Sheria ya majadiliano ya Watumishi wa Umma ilipitishwa na Bunge

    mwaka 2003 na ilitangazwa kwenye gazeti la Serikali mwaka 2004.

    Sheria hiyo inatumika ila haijaeleza wazi ni nani mwenye mamlaka ya kuunda

    chombo/baraza la majadiliano (joint staff council). Kufuatia hali hiyo ziliandaliwa

    kanuni ambazo zinatoa mwongozo kuhudu uundaji wa chombo cha majadiliano, na

    kanuni hizo zilitangazwa kwenye Gazeti la Serikali mwaka 2005. Kwa umuhimu wa

    suala hilo, naiagiza Menejimenti ya Utumishi wa Umma kukamilisha kanuni hizo ili

    zianze kutumika.

    Hata hivyo mie na nyie hatuna haja ya kungoja kanuni ndio tujadiliane masuala

    ya maslahi ya Taifa letu. Tuendeleeni.

    Ndugu Makamu wa Rais wa CWT, Ndugu Walimu,

  • Nimesema mengi. Naomba nimalizie kwa kuwapongeza tena walimu wote

    nchini kwa kazi nzuri mnayoifanya. Natambua mazingira magumu mnayofanyia kazi

    ila napenda kuwahakikishia dhamira yetu ya kuchukua hatua kuyaboresha. Nawasihi

    walimu wa ngazi zote nchini kufanya kazi kwa bidii, kuheshimu taaluma yenu na

    kuendelea kuwa kioo cha maadili mema kwa watoto tuliowakabidhi kufundisha na

    kwa Watanzania kwa ujumla. Hatma ya taifa hili ipo mikononi mwa Walimu.

    Nawashukuru tena kwa kunikaribisha kushiriki nanyi katika kilele cha Sherehe

    za Siku ya Mwalimu Duniani kwa mwaka huu wa 2006.

    Asanteni sana kwa kunisikiliza!